Nafasi Ya Matangazo

May 07, 2026

 
Serikali imeendelea kuongeza fursa za elimu nchini kwa kusajili shule 671 zikiwemo shule 23 za awali, shule 401 za awali na msingi, shule 245 za sekondari pamoja na vyuo viwili vya ualimu katika jitihada za kuboresha upatikanaji wa elimu kwa watoto na vijana nchini.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Prof. Mkenda amesema Serikali imeendelea kuwezesha ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya elimu ikiwemo mabweni sita katika shule za sekondari, madarasa 128, bwalo la chakula, nyumba ya mwalimu pamoja na ukarabati wa shule mbili za sekondari ili kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani.

Aidha, amesema Serikali imeimarisha uthibiti ubora wa elimu kwa kufanya tathmini ya jumla katika asasi 8,067 zikiwemo shule za awali, msingi, sekondari, vyuo vya ualimu, vituo vya elimu nje ya mfumo rasmi pamoja na Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi.

Ameeleza kuwa asasi zilizobainika kuwa na changamoto mbalimbali zilipewa ushauri wa kitaalamu ili kuboresha utoaji wa elimu.

Katika kuhakikisha upatikanaji wa vitabu vya kiada unaimarika, Waziri huyo amesema Serikali imechapa na kusambaza nakala 4,845,490 za vitabu vya darasa la tano pamoja na nakala 6,887,325 za vitabu na viongozi vya walimu kwa wanafunzi wa kidato cha pili.

Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, kwa masomo ya sanaa uwiano wa vitabu ni kitabu kimoja kwa wanafunzi watatu huku masomo ya sayansi yakifikia uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja.

Vilevile, Serikali imechapa na kusambaza nakala 3,000 za vitabu vya darasa la tano na nakala 31,520 za vitabu vya kidato cha pili kwa wanafunzi wenye uoni hafifu kwa uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja.

Kwa upande wa wanafunzi wasioona, amesema Serikali imechapisha na kusambaza nakala 9,600 za vitabu vya maandishi ya Breili kwa darasa la tano pamoja na nakala 8,362 za vitabu vya Breili kwa wanafunzi wa kidato cha pili ili kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji maalum wanapata haki sawa ya elimu. SOURCE: OKULY BLOG
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Serikali imeendelea kuweka mikakati madhubuti ya kukuza ubunifu, utafiti na matumizi salama ya teknolojia ya kisasa ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

Hatua hiyo inalenga kuongeza uwezo wa wananchi, taasisi za elimu pamoja na sekta mbalimbali kutumia teknolojia kwa tija na usalama zaidi.

Hayo yamebainishwa leo Mei 7,2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Katika juhudi za kukuza ubunifu, Serikali itaendeleza Mfuko wa Kibiashara wa Ubunifu  kwa lengo la kusaidia mawazo ya wabunifu na tafiti zenye manufaa kuingia kwenye matumizi ya kibiashara. Kupitia mpango huo, vyuo vitano vya Maendeleo ya Wananchi vitawezeshwa kuanzisha vituo vya ubunifu vitakavyotoa nafasi kwa vijana na wabunifu kukuza teknolojia, ujasiriamali na ajira.

“Serikali imejipanga kuimarisha uthibiti na utafiti wa kimkakati katika matumizi ya teknolojia ya nyuklia ili kuhakikisha usalama wa wananchi pamoja na mazingira. Mkakati huo unalenga kuongeza matumizi salama ya teknolojia hiyo katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii ikiwemo afya, kilimo na viwanda.”amesema Prof.Mkenda.

Katika mwaka ujao wa utekelezaji, Serikali itaendelea kudhibiti matumizi ya mionzi nchini kwa kufanya ukaguzi katika vituo 900 vyenye vyanzo vya mionzi. Ukaguzi huo unalenga kuhakikisha usalama wa wagonjwa, wafanyakazi, jamii pamoja na mazingira dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na matumizi yasiyo salama ya mionzi.

Vilevile, Serikali itapima na kudhibiti viwango vya mionzi kwa wafanyakazi 2,110 wanaofanya kazi kwenye mazingira yenye vyanzo vya mionzi ili kuhakikisha afya zao zinalindwa na viwango vya usalama vinafuatwa wakati wote.

Hatua hizi zinaonesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kuwekeza katika sayansi, teknolojia na ubunifu kama nyenzo muhimu ya kuharakisha maendeleo ya taifa na kuboresha maisha ya wananchi. SOURCE : Mzalendo Blog
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
 
Zaidi ya wanafunzi 3,021,177 wanatarajiwa kujiunga na elimu ya sekondari kidato cha kwanza ifikapo Januari 2028, kufuatia utekelezaji wa sera ya elimu ya lazima ya miaka 10 inayotekelezwa na Serikali kupitia Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Prof. Mkenda amesema idadi hiyo ya wanafunzi inatokana na wanafunzi waliopo darasa la tano na la sita mwaka 2026 ambao wanatarajiwa kuhitimu elimu ya msingi mwaka 2027 na kuanza sekondari mwaka 2028.

Amesema Serikali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeendelea na ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo madarasa, maabara, karakana pamoja na ununuzi wa vifaa na kuajiri walimu wapya ili kuhakikisha wanafunzi hao wanapokelewa kwa wakati.

Aidha, amesema utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka 10 ni hatua ya kihistoria itakayoongeza upatikanaji wa elimu ya sekondari na kusaidia kuandaa vijana wenye ujuzi na maarifa yanayokidhi mahitaji ya maendeleo ya taifa na ajira.

Amefafanua kuwa chini ya mfumo mpya wa elimu, mtoto atamaliza elimu ya lazima akiwa na umri wa miaka 16 tofauti na mfumo wa awali ambapo mwanafunzi alimaliza darasa la saba akiwa na miaka 13, umri ambao hauwezi kumwezesha kuajiriwa au kujiajiri.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, Serikali pia imeendelea na maandalizi ya kuanzisha mkondo wa amali katika shule za sekondari ili kuwajengea wanafunzi ujuzi wa kujitegemea na kukabiliana na changamoto za ajira.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaendelea na mapitio ya Sheria ya Elimu Sura ya 353 ambapo tayari maoni ya wadau mbalimbali yamekusanywa na taarifa ya awali ya mapitio hayo imeandaliwa.

Sambamba na hilo, Serikali imeandaa viunzi mbalimbali vya kuimarisha sekta ya elimu ikiwemo Kiunzi cha Umahiri wa Walimu katika TEHAMA 2026 pamoja na Kiunzi cha Kitaifa cha Ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa teknolojia za kidijitali katika sekta ya elimu. Source: OKULY BLOG 

Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini unaendelea kuwa wa uhakika na bidhaa hiyo haiadimiki.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Janeth Mahawanga Bungeni jijini Dodoma, aliyetaka kujua hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kukabiliana na athari za migogoro ya kimataifa na kidunia zilizopelekea changamoto ya mafuta nchini.

“Hatua ya kwanza ambayo Serikali imechukua ni kuhakikisha bidhaa hii haiadimiki. Zipo nchi ambazo tayari matatizo yameshajitokeza ya bidhaa hiyo kuadimika, hata kama una fedha hupati mafuta,” amesema Dkt. Nchemba.

Waziri Mkuu amesema Serikali imeanza taratibu za kuweka ruzuku ili kupunguza makali ya athari zinazotokana na hali inayoendelea Mashariki ya Kati.

Aidha, amesema Serikali imekaa na kuwasikiliza wadau mbalimbali, wakiwemo wadau wa usafirishaji, kwa lengo la kujadiliana namna ya kudhibiti ongezeko la gharama za usafirishaji.

“Tulikubaliana na wasafirishaji kupunguza baadhi ya gharama zinazotokana na hatua zinazochukuliwa na Serikali ambazo kimsingi si za lazima. Mfano, ulikuwepo uratibu wa mabasi yote ya mikoani kupita kila stendi, tumesema hakuna ulazima wa basi kupita kila stendi,” amesema Waziri Mkuu.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kusimamia sera, sheria na miongozo inayohusu afya na lishe ili kuhakikisha elimu inayotolewa kwa wananchi inalinda usalama wa afya za Watanzania.
 
Amesema hayo leo Alhamisi, Mei 7, 2026, wakati akijibu swali la Mbunge wa Hai, Mhe. Saashisha Mafuwe, katika kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu Bungeni jijini Dodoma. Mbunge huyo alitaka kujua mpango wa Serikali wa kuweka utaratibu maalumu wa utoaji elimu ya lishe kwa watu wenye taaluma husika.
 
Akijibu swali hilo, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kuhakikisha elimu ya afya na lishe inayotolewa kwa wananchi inazingatia taaluma, ushahidi wa kitaalamu na usalama wa afya.
 
“Serikali itaendelea kusimamia miongozo iliyopo ili taarifa au elimu inayotolewa na wenye taaluma ya lishe iwe ya kweli na imethibitishwa kutokuwa na madhara kwa kile kinachoshauriwa,” alisema.
 
Aidha, Waziri Mkuu aliielekeza Wizara ya Afya pamoja na mabaraza yanayosimamia taaluma za afya kuendelea kufanya tathmini kuhusu uratibu wa leseni na vibali kwa watoa elimu ya afya na lishe nchini.
 
Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu alisema Serikali inaendelea kufuatilia athari za migogoro ya kimataifa katika sekta mbalimbali za uchumi, hususan upatikanaji na bei ya mafuta.
 
Amesema hayo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Janeth Mahawanga, aliyetaka kujua hatua zinazochukuliwa na Serikali kukabiliana na athari za migogoro ya kimataifa zinazoathiri upatikanaji wa mafuta nchini.
 
Waziri Mkuu alisema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha bidhaa ya mafuta haipungui nchini na kupunguza athari za kupanda kwa gharama kwa wananchi.
 
“Mheshimiwa Spika, tayari kuna taratibu za namna ya kutekeleza zoezi hilo la ruzuku, ambapo zimekuwepo njia nyingi zinazotumika kwa ajili ya kuhakikisha tunapunguza makali ya madhara yanayotokana na kile kinachoendelea kule Mashariki ya Kati,” alisema.
 
Alisema Serikali pia imeendelea kushirikiana na wadau wa usafirishaji ili kudhibiti ongezeko la gharama za usafiri na usafirishaji.
 
“Tulizungumza na wadau wa usafirishaji na tukakubaliana kupunguza baadhi ya gharama walizokuwa wanazibeba. Kwa mfano, tulisema hakuna ulazima wa kila basi kupita kila stendi kama halina abiria wa kushusha,” alisema.
 
Aidha, alisema Serikali imepunguza baadhi ya taratibu za mizani kwa mabasi na magari ya usafirishaji ili kupunguza gharama za uendeshaji.
 
“Hata yale yanayotakiwa kupima uzito, tumepunguza vituo vya kupita kupima. Watapita kwenye mizani ya kwanza na ya mwisho kabla hawajamaliza safari,” alisema.
 
Alisema hatua hizo ni sehemu ya ruzuku zisizo za moja kwa moja zinazolenga kupunguza gharama ambazo zingebebwa na wananchi.
 
“Hizi ni njia mbalimbali za utoaji wa ruzuku zisizo za moja kwa moja ili kupunguza gharama ambazo zingebebwa na mwananchi,” alisema.
 
Waziri Mkuu alisema Serikali itaendelea kufuatilia mwenendo wa uchumi wa dunia na kuchukua hatua stahiki kuhakikisha huduma muhimu zinapatikana kwa wakati na kwa gharama nafuu kwa wananchi.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Kulia), akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule, katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule, akizungumza wakati akimkaribisha Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (hayupo pichani), kuhutubia kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.A
Mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Taifa, Bw. Ernest Mtondo, akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.

Baadhi ya wafanyabiashara wadogo maarufu kama wamachinga wa Soko la Mwenge, wakisikiliza hotuba ya Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (hayupo pichani), wakati wa  Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga pia kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.

Na. Joseph Mahumi, WF, Dar es Salaam
Serikali imewahakikishia wafanyabiashara wadogo maarufu kama wamachinga kuendelea kuboresha mazingira yao ya kufanyia biashara, ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kukuza uchumi jumuishi na kuongeza fursa za ajira nchini.

Ahadi hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akihutubia katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, uliolenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania madarakani pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.

Mhe. Mhandisi Munde alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara wadogo ili waweze kukuza mitaji yao na hatimaye kupanda daraja na kuwa wafanyabiashara wakubwa.

“Tunataka kuwaona mnapiga hatua kutoka biashara ndogondogo hadi kuwa wawekezaji wakubwa na Serikali yenu inatambua mchango wenu katika uchumi na itaendelea kuwaunga mkono,” alisema Mhe. Mhandisi Munde.

Aidha Mhe. Mhandisi Munde, alisisitiza kuwa maoni na mapendekezo yatokanayo na mkutano huo yatasaidia kuboresha sera na mifumo ya biashara nchini, sambamba na utekelezaji wa falsafa ya 4Rs (Maridhiano, Ustahimilivu, Mabadiliko na Kujenga upya) inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Aliongeza kuwa Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kurasimisha sekta isiyo rasmi, hatua itakayowezesha wafanyabiashara kupata fursa zaidi za mikopo nafuu, mafunzo na huduma nyingine muhimu za kiuchumi ikiwemo maeneo mazuri zaidi ya kufanya biashara kwa utulivu.

“Ni muhimu mkakubali kufanya kazi katika maeneo mtakayotengewa ili kurahisisha Serikali yenu kuwekeza miundombinu na huduma muhimu katika maeneo hayo na Pia, taasisi kama TRA na benki zitaendelea kuboresha huduma zao ili ziwe rafiki kwa wafanyabiashara wadogo,” alisisitiza Mhe. Mhandisi Munde.

Aidha Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule, pongezi za dhati kwa Wizara ya Fedha pamoja na taasisi zake kwa ushirikiano mkubwa wanaoendelea kuutoa kwa wafanyabiashara wadogo, ikiwemo juhudi za Mamlaka ya Mapato Tanzania -TRA katika kuonyesha uwajibikaji na mafanikio makubwa ya ukusanyaji mapato.

“Kwa dhati nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maono na jitihada zake za kufungua fursa za kiuchumi na kuimarisha miundombinu ya biashara, ikiwemo ujenzi wa masoko na maboresho ya maeneo ya biashara katika Wilaya ya Kinondoni, hasa kwa kutupa masoko zaidi ya 24 yakiwemo makubwa kama Tandale, na kuendelea kuboresha masoko mengine na kuongeza vibanda ili kuwawezesha wafanyabiashara wengi zaidi kufanya shughuli zao katika mazingira bora na salama” alisema Bw. Mtambule

Naye Mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Taifa, Bw. Ernest Mtondo alisema kuwa, Wamachinga wanatambua na wanathamini juhudi za Serikali katika kuboresha mazingira ya biashara, pamoja na jitihada za kuimarisha zaidi mifumo ya hifadhi ya jamii kwa wajasiriamali hao.

Bw. Mtondo aliishukuru Wizara ya Fedha kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuanza kuweka mazingira rafiki ya biashara, ikiwemo ujenzi wa mahema katika maeneo maalum ambayo yatabeba zaidi ya wamachinga 300, hatua ambayo imeanza kuleta utulivu na heshima kwa shughuli za wamachinga.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Taifa, Bw. Joseph Mwanakijiji, amesema kuwa kuanzishwa kwa shirikisho hilo kumelenga kuwaunganisha wamachinga na wafanyabiashara ndogondogo nchini kote, huku likikuza ushirikiano thabiti kati yao na Serikali.

Bw. Mwanakijiji alisema kuwa kupitia SHIUMA, wamachinga wameanza kunufaika na fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwemo upatikanaji wa mikopo kutoka taasisi za kifedha, pamoja na kupendekeza na kurasimisha maeneo rafiki ya biashara.

“Tayari kumekuwepo na maboresho makubwa ikiwemo ujenzi wa masoko maalum kama Machinga Complex Dodoma, kuimarika kwa mahusiano na Serikali, pamoja na kuboreshwa kwa mazingira ya biashara katika maeneo mbalimbali kama Mwenge na tunaahidi kuongeza ushirikiano na TRA katika ukusanyaji wa mapato pamoja na kuwahamasisha zaidi wamachinga kujiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii kama NSSF ili kujenga ustawi wao wa baadaye” alisema Bw. Mwanakijiji.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Kamishna Msaidizi wa Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi Emma Komba, akizungumza wakati akifungua kikao kazi cha kufanya mapitio ya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, kwa lengo la kuioanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Sheria Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Paul Kadoshi, akifafanua jambo kuhusiana na mchakato wa zabuni, katika kikao kazi cha kufanya mapitio ya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, kwa lengo la kuioanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dar es Salaam.
Mwanasheria kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Bi. Asimuna Kipingui, akitoa maoni katika kikao kazi cha kufanya mapitio ya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, kwa lengo la kuioanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dar es Salaam.
Mchambuzi wa Sera wa Shirikisho la Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Bw. Michael Kijavara, akitoa maoni katika kikao kazi cha kufanya mapitio ya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, kwa lengo la kuioanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya wadau wakifuatilia hoja zilizokuwa zikiwasilishwa katika kikao kazi cha kufanya mapitio ya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, kwa lengo la kuioanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dar es Salaam.
************
Na. Saidina Msangi, WF, Dar es Salaam.
Wizara ya Fedha imeendelea na mchakato wa kupitia upya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, kwa lengo la kuioanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kupitia kikao kazi kilichowakutanisha wadau mbalimbali kutoka sekta ya umma na binafsi.
 
Wizara imeendelea na mchakato huo ikiwa ni kikao kazi cha pili kufanyika ambapo wadau mbalimbali walipata fursa ya kutoa maoni na mapendekezo yatakayosaidia kuboresha Sheria hiyo, katika kikao kazi kilichofanyika ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dar es Salaam.
 
Akizungumza wakati akifungua kikao hicho, Kamishna Msaidizi wa Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi Emma Komba, alisema mapitio hayo yanalenga kujenga mfumo wa kisasa unaojumuisha hatua zote za mnyororo wa ugavi, kuanzia upangaji wa mahitaji, ununuzi, upokeaji na ugomboaji, uhifadhi na utunzaji, usambazaji, hadi uondoshaji wa mali.
 
Alisisitiza kuwa mapitio hayo ni hatua ya kimkakati ya kuhakikisha kuwa masuala yote yanayohusu mnyororo mzima wa ugavi yanajumuishwa kikamilifu katika Sheria mpya, na kwamba mageuzi hayo yatakuwa chachu ya kuchochea maendeleo ya Taifa.
 
Bi. Komba aliwahimiza wadau wote kushiriki kikamilifu kutoa maoni na kukisisitiza kuwa ushiriki wao ndio utakaohakikisha Sheria mpya inakuwa bora, jumuishi na yenye tija kwa maendeleo ya Taifa kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo 2050.
 
Kikao hicho, kilichoratibiwa na Wizara ya Fedha kupitia Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, kiliwakutanisha pamoja wadau mbalimbali kutoka Sekta ya umma na binafsi.
 
Kwa upande wa sekta ya umma, taasisi zilizoshiriki ni pamoja na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini (GPSA), TANROAD, SUMAJKT pamoja na Benki ya Maendeleo ya TIB.
 
Kwa upande wa sekta binafsi, walishiriki walikuwa Benki ya NBC, Soft tech consultancy, Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Cross World Travel Agent Limited, Masasi Construction, pamoja na Perfect Infotech International, ambao walipata fursa ya kuwasilisha maoni yao kuhusu namna ya kuboresha mazingira ya biashara na ushiriki wao hasa kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kushiriki katika shughuli za ununuzi wa umma na ugavi.

Kamishna Msaidizi wa Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi. Emma Komba, akiwa katika picha ya pamoja na wadau walioshiriki katika kikao kazi cha kutoa maoni na kufanya mapitio ya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, kwa lengo la kuioanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dar es Salaam.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam.)
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kwenye picha na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde, pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Perseus Mining Limited Bw. Rick Menell mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu ya Chamwino, Dodoma tarehe 06 Mei, 2026. 

Perseus Mining Limited ni mwekezaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga, Wilayani Sengerema, Mkoani Mwanza kupitia Kampuni ya Sotta Minining Corporation Limited, inayomilikiwa kwa ubia na Serikali ya Tanzania. 
***********
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amekutana na kuzungumza na uongozi wa Kampuni ya Perseus Mining Limited, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma. 

Ujumbe huo uliongozwa na Mwenyekiti wa Kampuni hiyo, Bw. Rick Menell, aliyeambatana na Mjumbe wa Bodi ya Kampuni ya Sotta Mining Corporation Limited, Prof. Raphael Chibunda, katika mazungumzo yaliyolenga kujadili maendeleo ya Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga uliopo wilayani Sengerema, mkoani Mwanza. 

Mradi huo wenye thamani ya dola za Marekani milioni 523 (zaidi ya shilingi trilioni moja) tayari umeingia katika hatua kamili ya ujenzi, na unatarajiwa kuanza uzalishaji katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka 2027, ukiwa ni mgodi mkubwa wa kwanza mpya wa dhahabu kuanzishwa nchini takribani miaka 20 iliyopita. 

Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga unatekelezwa na Kampuni ya Sotta Mining Corporation Limited, ambayo ni ubia baina ya Kampuni ya Perseus Mining Limited yenye umiliki wa asilimia 80, na Serikali ya Tanzania inayomiliki asilimia 20 ya hisa. 

Hadi mwezi Februari, 2026, makadirio ya akiba ya madini katika eneo la mradi yalikuwa wakia milioni 4.0, sawa na ongezeko la asilimia 73 kutoka wakia milioni 2.3 za awali, na hivyo kuongeza makisio ya uhai wa mgodi huo hadi kufikia miaka 16. 

Mradi huo unatarajiwa kuzalisha wastani wa wakia 200,000 za dhahabu kwa mwaka, na kufikia kilele cha uzalishaji wa wakia 250,000 mwaka 2028. 

Kazi za maandalizi ya mgodi zinaendelea, sambamba na ujenzi wa kambi ya kudumu ya wafanyakazi, inayotarajiwa kukamilika katikati ya mwaka 2026, huku ujenzi wa nyumba za wananchi wa maeneo yaliyopitiwa na mradi zikiwa katika hatua za mwisho kukamilika, chini ya mpango wa uhamaji na fidia. 

Rais Dkt. Samia amepongeza uwekezaji huo mkubwa, akisema unaonesha kuimarika kwa sekta ya madini na nafasi yake katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa. 

Amesisitiza kuwa mradi huo unapaswa kuleta manufaa ya moja kwa moja kwa Watanzania, hususan jamii zinazozunguka eneo la mgodi, kupitia ajira, usambazaji wa bidhaa na huduma mgodini, pamoja na utekelezaji wa miradi ya kijamii. 

Aidha, amesema Serikali inataka kuona ushiriki wa Watanzania katika mnyororo wa thamani wa mradi huo, ili uwekezaji mkubwa unaofanyika katika sekta ya madini ufungue fursa za kiuchumi kwa wananchi. 

Rais Dkt. Samia ameongeza kuwa, Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini ili kuvutia mitaji zaidi katika sekta ya madini na maeneo mengine ya kimkakati, huku akizielekeza taasisi zinazohusika na uwekezaji kushughulikia kwa haraka changamoto zinazowakabili wawekezaji nchini. 

Kwa upande wao, wawakilishi wa kampuni ya Perseus Mining Limited wameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji, wakiahidi kushirikiana na Serikali katika kuleta mabadiliko makubwa ya miundombinu na teknolojia katika mnyororo wa uzalishaji wa dhahabu nchini.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde kwenye picha na Ujumbe wa Kampuni ya Perseus Mining Limited na Sotta Minining Corporation Limited mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu ya Chamwino, Dodoma tarehe 6 Mei, 2026.

Perseus Mining Limited ni mwekezaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga, Wilayani Sengerema, Mkoani Mwanza kupitia Kampuni ya Sotta Minining Corporation Limited, inayomilikiwa kwa ubia na Serikali ya Tanzania. 
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments

May 06, 2026

Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi akila kiapo kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 06 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 06 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amemuapisha Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi (Mb.) kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, katika hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma.
 
Rais Dkt. Samia amesema uteuzi wa Dkt. Munisi, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa NCCRMageuzi, umetokana na sifa, uwezo na uzoefu wake katika masuala ya umma na mahusiano, akisema Watanzania wote wana wajibu wa kuunganisha nguvu katika kulitumikia Taifa bila kujali tofauti za itikadi za vyama.
 
“Evaline ni Katibu Mkuu wa chama cha upinzani cha NCCR-Mageuzi; lakini nimeangalia wasifu wake, nikaona ana sifa za kuingia ndani ya Serikali na kutusaidia,” amesema Rais Dkt. Samia.
 
Halikadhalika, amemtaka Dkt. Munisi kushirikiana na viongozi na watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano kusimamia kazi zenye staha, haki na stahiki za wafanyakazi katika sekta ya umma na binafsi, pamoja na juhudi za kutafuta na kulinda fursa za ajira kwa vijana wa Tanzania nje ya nchi. 

Amesema Ofisi hiyo pia ina jukumu la kuimarisha mahusiano kati ya Serikali, waajiri na waajiriwa, pamoja na mahusiano ya kuheshimiana baina ya Serikali na mihimili mbalimbali ya dola. 

Kwa upande wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), Rais Dkt. Samia amemtaka Mtendaji Mkuu Dkt. Kheri Mahimbali kusimamia vyema taasisi hiyo ili kurejesha ufanisi na imani yake kwa umma, hususan baada ya hoja na changamoto zilizoibuliwa katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Rais Dkt. Samia amewataka viongozi hao kutekeleza majukumu yao kwa nidhamu, unyenyekevu na matokeo, akisisitiza kuwa dhamana ya uongozi inapaswa kuelekezwa katika kutatua changamoto za wananchi. 
“Vyeo ni dhamana. 
Mungu amekuweka hapo ili utumikie watu,” amesema Rais Dkt. Samia. 

Viongozi wengine walioapa kiapo cha uadilifu kwa watumishi wa umma ni: Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Ndugu Kheri Abdul Mahimbali; Katibu wa Rais, Balozi Ali Jabir Mwadini; Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mhandisi Peter Philip Mwasalyanda; Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabir Kuwe Bakari; na Mshauri wa Rais, Masuala ya Jamii, Mhe. Angela Charles Kizigha (Mb.)
Viongozi mbalimbali wakiapa kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026. Kutoka kulia ni; Ndugu Kheri Abdul Mahimbali Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Balozi Ali Jabir Mwadini, Katibu wa Rais, Mhandisi Peter Phillip Mwasalyanda Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabir Kuwe Bakari Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Mhe. Angela Charles Kizigha, Mshauri wa Rais, Masuala ya Jamii
Viongozi mbalimbali wakiapa kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026. Kutoka kulia ni; Ndugu Kheri Abdul Mahimbali Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Balozi Ali Jabir Mwadini, Katibu wa Rais, Mhandisi Peter Phillip Mwasalyanda Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabir Kuwe Bakari Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Mhe. Angela Charles Kizigha, Mshauri wa Rais, Masuala ya Jamii
Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya Uapisho wa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.


Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya Uapisho wa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali mara baada ya kumuapisha Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali mara baada ya kumuapisha Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azzan Zungu, Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji Sivangilwa Mwangesi katika picha na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.

Posted by MROKI On Wednesday, May 06, 2026 No comments

May 05, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto wakati wakitembelea mabanda ya maonesho kabla ya kushiriki kwenye Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Kenya lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia viongozi pamoja na wafanyabiashara kwenye Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Kenya lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam tarehe 04 Mei, 2026. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia viongozi pamoja na wafanyabiashara kwenye Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Kenya lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam tarehe 04 Mei, 2026. 

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akihutubia viongozi pamoja na wafanyabiashara kwenye Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Kenya lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026. 
Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akihutubia viongozi pamoja na wafanyabiashara kwenye Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Kenya lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.
 


Viongozi pamoja na wafanyabiashara wakiwa kwenye Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Kenya lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026. 


Posted by MROKI On Tuesday, May 05, 2026 No comments

May 04, 2026

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na washiriki wa Mkutano Mkuu wa 11 na Kongamano la Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki (EAAP), unaofanyika katika Ukumbi wa Blue Sapphire, jijini Dar es Salaam, leo tarehe 4 hadi 6 Mei, 2026. 

***************
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema ushirikiano wa kikanda na kimataifa ni sharti la mafanikio katika mapambano dhidi ya uhalifu wa kimataifa unaozidi kubadilika na kuvuka mipaka.

Amesema kuwa katika dunia ya sasa, aina nyingi za uhalifu hupangwa, hufadhiliwa na kuratibiwa kwa njia za kidijitali, hali inayohitaji mifumo imara ya kiteknolojia pamoja na ushirikiano wa pamoja ili kuudhibiti kwa ufanisi.

Ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, Mei 4, 2026, wakati akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa 11 na Kongamano la Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki (EAAP), unaofanyika katika Ukumbi wa Blue Sapphire, jijini Dar es Salaam, kuanzia tarehe 4 hadi 6 Mei, 2026, wenye kaulimbiu isemayo “Matumizi ya Teknolojia katika Kukabiliana na Uhalifu Dhidi ya Wanyamapori na Uhalifu wa Kimataifa Uliopangwa.”

“Kama ambavyo uhalifu uliopangwa hauwezi kuwepo bila kuvuka mipaka, vivyo hivyo vyombo vya dola na mifumo ya haki ya jinai haviwezi kukabiliana nao kwa ufanisi bila kuwa na mifumo madhubuti ya ushirikiano wa kimataifa, hususan katika maeneo ya msaada wa kisheria na urejeshaji wa watuhumiwa,” alisema.

Akifafanua zaidi kuhusu mwelekeo wa uhalifu wa kisasa, Waziri Mkuu alisema:

“Utafiti unaonesha kuwa katika hali nyingi, uhalifu dhidi ya wanyamapori na uhalifu wa kimataifa hupangwa kidijitali, hufadhiliwa kwa njia za kielektroniki na kuratibiwa kuvuka mipaka, na pia hufichwa kwa kutumia mbinu tata za kiteknolojia, hali inayofanya mipango na athari zake kuvuka mipaka kwa kasi kubwa ambayo wakati mwingine hupita bila kugundulika.”

Alisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ni sehemu muhimu ya mafanikio katika mapambano hayo.

“Katika mazingira haya, hatuwezi kufanikiwa katika mapambano dhidi ya uhalifu wa kimataifa uliopangwa bila kutumia kikamilifu teknolojia kama nyenzo muhimu katika kukabiliana na changamoto hii ndani ya ukanda wa Afrika Mashariki na duniani kwa ujumla,” alisema.

Akizungumzia athari za uhalifu huo, Waziri Mkuu alisema ni tishio kwa uchumi na usalama wa mataifa.

“Ni dhahiri kwamba biashara haramu ya wanyamapori na aina nyingine za uhalifu wa kimataifa uliopangwa ni tishio kubwa kwa mataifa yetu; unachangia kupotea kwa rasilimali zetu na pia ni tishio kwa utulivu na usalama wa nchi zetu,” alisema.

Akielezea hatua zilizochukuliwa na Tanzania, Waziri Mkuu alisema Serikali imeendelea kuboresha mifumo ya kisheria ili kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.
“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikipitia na kuboresha sheria zake za msaada wa kisheria ili kupanua wigo wa ushirikiano, ikiwemo matumizi ya ushahidi wa kidijitali, ufuatiliaji wa mawasiliano na mbinu za kisasa za uchunguzi,” alisema.

Aidha, alibainisha kuwa Serikali imeondoa baadhi ya taratibu za urasimu ili kuwezesha utekelezaji wa haraka wa maombi ya msaada wa kisheria kupitia mamlaka husika.

Waziri Mkuu alizitaka nchi wanachama kutumia jukwaa la EAAP kama chombo cha kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kubadilishana taarifa.
“Katika dunia ya sasa ambapo uhalifu hauna mipaka, majibu yetu lazima yawe ya pamoja, ya kimkakati na yenye mshikamano,” alisema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainabu Katimba, alisema uwepo wa Waziri Mkuu katika mkutano huo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika mapambano dhidi ya uhalifu.

Alisema kaulimbiu ya mkutano huo ni ya wakati muafaka na inaakisi changamoto za sasa, akiwahimiza washiriki kutumia jukwaa hilo kubadilishana uzoefu na kuimarisha mifumo ya haki katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Naye Rais wa Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki (EAAP), ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mashtaka wa Jamhuri ya Kenya, Renson Ingonga, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano na matumizi ya teknolojia katika kukabiliana na uhalifu unaobadilika kwa kasi.

Alisema mkutano huo ni fursa ya kujenga mitandao imara ya kitaaluma, kuimarisha uaminifu na kukuza mifumo ya ushirikiano itakayowezesha kukabiliana ipasavyo na uhalifu wa kimataifa uliopangwa.

Mkutano huo wa kimataifa unawakutanisha Wakurugenzi wa Mashtaka, Mawakili Wakuu wa Serikali, viongozi wa vyombo vya sheria pamoja na wadau kutoka mashirika ya kikanda na kimataifa kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na mifumo ya haki jinai katika kukabiliana na uhalifu wa kuvuka mipaka.

Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki (EAAP) kinaundwa na nchi wanachama ambazo ni Tanzania, Burundi, Ethiopia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Kenya, Msumbiji, Rwanda, Seychelles, Sudan Kusini, Somalia, Malawi, Sudan, Zambia na Uganda.

Akihitimisha, Waziri Mkuu aliwataka washiriki kuhakikisha mkutano huo unazaa matokeo yenye tija kwa ukanda wa Afrika Mashariki.
“Kwa maneno hayo machache, natangaza rasmi kufunguliwa kwa Mkutano Mkuu wa 11 na Kongamano la Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki,” alisema.
Posted by MROKI On Monday, May 04, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo