Nafasi Ya Matangazo

June 25, 2026

IMG_6244.JPG
Benki ya NMB imetangaza udhamini wa Sh milioni 150 kufanikisha msimu wa nane wa Mashindano ya Kombe la Mkuu wa Majeshi—CDF Cup 2026—yatakayofanyika Dar es Salaam kuanzia Julai 6 hadi 17.

Mashindano hayo yatahusisha michezo 13 na timu kutoka Kamandi ya Makao Makuu ya JWTZ, Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Kamandi ya Jeshi la Anga, Kamandi ya Jeshi la Wanamaji, Kamandi ya Jeshi la Akiba na Kamandi ya Jeshi la Kujenga Taifa.

Mkuu wa Idara ya Wateja Binafsi wa Benki ya NMB, Aikansia Muro, alisema udhamini huo unaendeleza ushirikiano wa benki hiyo na majeshi katika kukuza michezo, kuimarisha ushindani na kujenga umoja, afya thabiti na mshikamano miongoni mwa washiriki.

Mashindano yatafunguliwa Julai 6 katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, huku yakitarajiwa kutoa jukwaa la kukuza vipaji, kuimarisha utimamu wa mwili na afya ya akili pamoja na kujenga mahusiano mema kwa washiriki.

Mkuu wa Idara ya Wateja Binafsi wa Benki ya NMB, Aikansia Muro (kushoto), akikabidhi hundi mfano ya udhamini wa Sh milioni 150 kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya CDF Cup 2026, Brigedia Jenerali Saidi Hamis Saidi (katikati), jijini Dar es Salaam.

Mashindano hayo yatafanyika kuanzia Julai 6 hadi 17, yakishirikisha timu za kijeshi katika michezo 13.
IMG_6259.JPG
IMG_6246.JPG

IMG_6247.JPG

IMG_6248.JPG

IMG_6250.JPG

IMG_6251.JPG

IMG_6253.JPG

IMG_6254.JPG

IMG_6255.JPG

IMG_6257.JPG

IMG_6258.JPG

IMG_6245.JPG
Posted by MROKI On Thursday, June 25, 2026 No comments
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hania Bwahama akimuelezea Mshiriki wa mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) kutoka nchini Nigeria Mya Nyon vifaa vinavyotumika wakati wa upasuaji wa moyo alipotembelea banda la JKCI lililopo katika mkutano huo unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) kilichopo jijini Dar es Salaam.
Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Alex Msoka akimuelezea Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu kwa Umma Dkt Rahma Hingora kuhusu kampeni ya Jua Namba Zako inayofanywa na Taasisi hiyo alipotembelea banda la JKCI wakati wa mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) kilichopo jijini Dar es Salaam.
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hania Bwahama akimuelezea mtaalamu wa afya kutoka nchini Afrika Kusini Roylah Rykiel kuhusu huduma za upasuaji wa moyo zinazotolewa na Taasisi hiyo wakati wa mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) kilichopo jijini Dar es Salaam.
**************
Watalaamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wameshiriki katika mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) ili kujadili changamoto mbalimbali zinazokwamisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza na kufikia maamuzi ya pamoja yatakayosaidia kufanikisha malengo ya afya kuelekea dira 2050.
Akizungumza wakati wa mkutano huo  Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Alex Msoka alisema mkutano huo umesaidia kuwakutanisha wadau mbalimbali  kutoka nchi za Afrika  kujadili kwa pamoja na kuweka mikakati ya kukabiliana na magonjwa hayo.
Dkt. Msoka alisema magonjwa yasiyoambukiza yanaongezeka kwa kasi katika Bara la Afrika jambo linalohitaji hatua za haraka na ushirikiano wa wadau mbalimbali katika kuyadhibiti.
“JKCI kama mdau katika mkutano huu tunashiriki kikamilifu katika kujadili changanmoto zilizopo na kutafuta suluhisho zake ili kuimarisha utoaji wa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kwani takwimu zinaonesha kuwa asilimia 35 ya vifo nchini vinatokana na magonjwa hayo”, alisema Dkt. Msoka.
Dkt. Msoka alisema kupitia mkutano huo JKCI imeweka banda la maonesho kuwaonesha wataalamu kutoka nchi washiriki wa mkutano huo huduma inazozitoa na namna ambavyo imeleta mabadiliko makubwa katika matibabu ya moyo Afrika Mashariki na Kati.
“Kumekuwa na changamoto nyingi zinazotokana na mtindo usiofaa wa maisha katika ukanda wetu kama vile kutokufanya mazoezi, matumizi ya pombe kupita kiasi na kutokufuata lishe bora, hizi ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia magonjwa yasiyoambukiza, hivyo sisi kama JKCI tunaendelea kupambana na magonjwa hayo katika jamii yetu”, alisema Msoka.
Baadhi ya washiriki wa mkutano huo waliotembelea banda la JKCI walipongeza jitihada za Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha huduma za afya hususani huduma bingwa bobezi za magonjwa ya moyo.
“Huduma zinazotolewa na JKCI ni huduma za kiwango cha juu, naiomba Serikali iendelee kutoa elimu kwa wananchi wake hususani walioko vijijini ili wanapokumbana na changamoto za magonjwa ya moyo waweze kupata huduma kwa wakati”, alisema Padri Cosmas Mgina wa Kanisa la Anglikana Tanzania Dayosisi ya Dar es Salaam.
Kwa upande wake Daktari kutoka nchini Ghana Wallace Ollen alisema JKCI imekuwa mfano wa kuigwa barani Afrika kwa kutoa huduma za kibingwa bobezi za matibabu ya magonjwa ya moyo na mishipa ya damu.
“Naipongeza JKCI kwani upatikanaji wa huduma za matibabu ya moyo Barani Afrika umekuwa msaada mkubwa kwa wananchi wetu kwa kuwa sasa hatuna sababu ya kusafiri kwenda mataifa mengine kama India kupata matibabu bingwa ya moyo”, alisema Dkt. Ollen.
Posted by MROKI On Thursday, June 25, 2026 No comments
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Chemba amesema michezo ya watu wenye ulemavu imeiletea heshima kubwa Tanzania kimataifa katika nyanja ya michezo.
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu ameeleza hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Yumna Mmanga aliyetaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inasimamia michezo ya watu wenye ulemavu iweze kushinda medali ambapo Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika michezo ya watu wenye ulemavu ili kuitangaza zaidi Tanzania.
“Ni kweli timu zetu zimekuwa zikishiriki mashindano mbalimbali ya watu wenye ulemavu, na kweli hazijafanikiwa kuleta medali, lakini kwa kweli wameiletea sifa kubwa nchi yetu,” amesema Waziri Mkuu.
“Kama Waheshimiwa Wabunge mtakumbuka, timu yetu ya Tembo Warriors ilishiriki Kombe la Dunia mwaka 2022 nchini Uturuki, na tena haikushiriki kinyonge, ilishiriki kama timu iliyojiandaa na ilionesha mchezo mzuri sana, kadhalika ikashiriki michuano ya AAFCON ya wenye ulemavu mwaka 2024 nchini Misri, pamoja na michuano ya CECAFA ya wenye ulemavu ya mwaka huu nchini Burundi, ambako ilifika fainali, siyo jambo dogo,” ameongeza Dkt. Mwigulu.
Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kutengeneza mazingira ya kuhakikisha timu mbalimbali zinatwaa medali, ikiwemo kutengeneza miundombinu ya michezo ya watu wenye ulemavu na kusajili timu na wachezaji wa michezo ya watu wenye ulemavu.
“Pamoja na kwamba kwenye yale mashindano timu zetu hazikupata medali nyingi, lakini bado wachezaji wa timu zile waliweza kuonekana duniani na kusajiliwa na timu mbalimbali, Serikali itaendelea kuwekeza katika michezo hiyo ili kuhakikisha timu zetu zinapata mafanikio zaidi,” amesisitiza Waziri Mkuu.
Posted by MROKI On Thursday, June 25, 2026 No comments

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameiagiza Benki Kuu ya Tanzania, vyombo vya dola na taasisi nyingine zinazosimamia sheria, kudhibiti matumizi ya sarafu za kigeni katika uuzaji na ununuzi wa bidhaa na huduma nchini kwani ni kinyume cha Sheria.
“Sarafu rasmi kwa malipo halali ndani ya nchi yetu ni Shilingi ya Kitanzania, ni jambo la kisheria na ni jambo la kikatiba, kwa muongozo tulioutoa, malipo yote, kunukuu bei na matangazo yafanyike kwa shilingi ya Kitanzania”, amesema Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Alhamisi, Juni 25, 2026) Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Suma Fyandomo.
Fyandomo alitaka kujua mikakati ya Serikali katika kusimamia matumizi ya Shilingi ya Kitanzania katika huduma zote za kifedha nchini, ambapo Waziri Mkuu amesema matumizi holela ya sarafu isiyo ya Kitanzania ni kuvunja sheria.
“Wale wanaoweka bei za viwanja, ada, upangishaji wa nyumba, uuzaji wa huduma na maeneo mengine kwa dola au sarafu nyingine za kigeni wajue wanakiuka sheria yetu, na kwa kweli hawaitendei uzalendo nchi yetu ya Tanzania,” amesema Dkt. Mwigulu.
“Wengine wanafanya utakatishaji wa fedha chafu kwa kutangaza bei kwa sarafu za kigeni ili baadaye waonekane waliuza viwanja, lakini ni michezo michafu tu,” ameongeza Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu amesisitiza kuwa kupitia muongozo uliotolewa na Serikali, hata taasisi za Serikali zimeacha matumizi ya sarafu za kigeni katika manunuzi na utoaji wa huduma na kuzitaka mamlaka kukomesha matumizi ya sarafu hizo za kigeni kinyume cha sheria.
“Nielekeze taasisi zetu zinazosimamia sheria, Benki Kuu ya Tanzania na Vyombo vya Dola, tuendelee kufuatilia mienendo ya aina hii, ili wale watakaotaka kunukuu bei ama kuuza bidhaa kwa fedha za kigeni ili kuficha mambo mengine ikiwemo utakatishaji wa fedha haramu, tudhibiti vitu vya aina hiyo kwa sababu ni kinyume cha sheria,” amesema Dkt. Mwigulu.
Katika hatua nyingine, Katika hatua nyingine Dkt. Mwigulu amezielekeza halmashauri ambazo ziko kando ya maeneo yanayoweza kutumika kwa ajili ya kuweka vizimba vya ufugaji wa samaki watumie fursa hiyo kuwawezesha wanawake kujihusisha na ufugaji huo kwa kutumia mapato ya ndani ya halmashauri.
“Tumieni ule utaratibu wa asilimia 4:4:2 ili kuweza kuwawezesha wanawake kushiriki katika uvuvi wa kutumia vizimba katika maeneo ambayo fursa hiyo ipo”
Waziri Mkuu ameeleza hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Lucy Mwakyembe aliyetaka kufahamu Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha wanawake kupata vizimba vya kuzalishia samaki katika maeneo yote ya bahari, mito na maziwa ambapo Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na mikakati mbalimbali ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kupitia sekta ya uvuvi, na wanawake wakiwa ni miongoni mwa wanufaika.
“Takriban miaka miwili au mitatu iliyopita, Mheshimiwa Rais alizindua zoezi la kugawa vizimba kwa vijana wa Tanzania. Zoezi hilo linahusisha vijana wote wa kike na wa kiume, kwa hiyo zoezi hilo lilihusisha pia wanawake,” ameeleza Dkt. Mwigulu.
Waziri Mkuu ameongeza kuwa, kwa upande wa bahari na maeneo mengine zoezi hilo linaendelea, likiwa linafanyika kwa majaribio, na  uwekezaji mkubwa wa bandari ya uvuvi iliyopo wilayani Kilwa, utachochea zaidi mpango huo kwa kuwa kutakuwa na mahitaji makubwa ya malighafi.
“Mheshimiwa Mbunge nakuhakikishia, Serikali inaweka mkazo katika jambo hilo, na kule tunakokwenda utakuwa ni uvuvi wa kawaida katika maeneo mengi ili kuweza kuwawezesha vijana na wanawake wengi pamoja na makundi maalum kujihusisha na shughuli hizo,” amesisitiza Waziri Mkuu.

Posted by MROKI On Thursday, June 25, 2026 No comments

June 24, 2026


Na Mwandishi Maalumu – Dodoma
Jumla ya watu 546 wamefanyiwa uchunguzi wa afya kwa kupimwa Namba Zao wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi wa afya iliyokuwa ikifanyika katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma.
Kupitia kambi hiyo iliyomalizika leo katika Viwanja vya Chinangali Park vilivyopo jijini Dodoma watu waliotembelea katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) walifanyiwa vipimo vya kuchunguza ugonjwa wa shinikizo la damu, kiwango cha sukari kwenye damu, uwiano wa urefu kwa uzito pamoja na mzunguko wa kiuno.
Aidha watu 192 walifanyiwa kipimo cha kuchunguza utendaji kazi wa moyo (Echocardiography – ECHO), huku watu 11 wakifanyiwa kipimo cha kuangalia mfumo wa umeme wa moyo (Electrocardiography – ECG).
Akizungumza wakati wa kuhitimisha kambi hiyo Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Daud Gwilenza alisema watu 94 wamepewa rufaa kwenda katika Taasisi hiyo kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
“Watu 82 tumewabaini kuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu, huku watu 20 tumewabaini kuwa na tatizo la sukari. Baadhi ya watu hawa walikuwa tayari wanajua hali zao lakini wengine hawakuwa wanajua kama wana matatizo ya shinikizo la damu na sukari”, alisema Dkt. Daud.
Dkt. Daud aliongeza kuwa magonjwa mengine yaliyobainika kupitia kambi hiyo ni pamoja na kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo na kutanuka kwa moyo hali ambayo kwa kiasi kikubwa husababishwa na shinikizo la damu la muda mrefu.
“Jamii inapaswa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara, hii itatusaidia kulinda afya zetu na kuchukua hatua mapema tunapogundulika kuwa na magonjwa yasiyoambukiza ambayo kwa sasa yanaongezeka kwa kasi katika jamii yetu”, alisema Dkt. Daud.
Kwa upande wao wananchi waliopata huduma katika banda la JKCI waliishukuru Serikali kwa kuwezesha kufanyika kwa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mkoani Dodoma jambo lililowapa fursa ya kufanyiwa uchunguzi wa afya bila gharama.
James Balilonga mkazi wa Dodoma alisema maonesho hayo yamemsaidia kutambua umuhimu wa kufanya uchunguzi wa afya hata pale mtu anapokuwa hana dalili za ugonjwa.
“Unapokutana na wataalamu wa afya na kupata elimu kuhusu umuhimu wa kuchunguza  afya unahamasika kuchukua hatua. Hili limekuwa fundisho kwangu kwamba siyo lazima nisubiri kuumwa ndipo nifanye uchunguzi wa afya”, alisema James.
Naye Doris Mwirezeyo alizitaka taasisi za afya kuanzia ngazi ya Wilaya kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuchunguza afya mara kwa mara ili kuwasaidia wananchi kujikinga na magonjwa na kupata matibabu kwa wakati.
“Leo nimejifunza jambo muhimu, kama tungekuwa na utamaduni wa kupima afya mara kwa mara na kuzingatia mtindo bora wa maisha pengine tusingekuwa na wagonjwa wengi wenye matatizo ya moyo, elimu hii inapaswa kuwafikia wananchi hadi ngazi za chini ili waweze kujilinda”, alisema Doris.

Posted by MROKI On Wednesday, June 24, 2026 No comments
Na: Dkt. Reubeni Lumbagala 
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ni chombo muhimu nchini katika kuhakikisha mipango na mikakati ya maendeleo inatimizwa kikamilifu. Hii inatokana na ukweli kuwa mipango mingi ya maendeleo kama uboreshaji wa sekta za elimu, afya, maji, masoko, viwanda, umeme, barabara, makazi, biashara, inategemea upatikanaji wa raslimalifedha ili ziwezeshe utekelezaji wake.

TRA ina wajibu wa kukusanya kodi kutoka kwa walipakodi wake kama wafanyabiashara, wawekezaji, wafanyakazi na wajasiriamali mbalimbali. Mafanikio ya ukusanyaji kodi, ndiyo msingi wa kuiwezesha serikali kutimiza mipango yake ya maendeleo kwa ustawi na maendeleo ya wananchi.

Sasa TRA imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake. TRA imepata mafanikio makubwa sana hasa katika uongozi wa serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Rais Dk. Samia aliweka msingi wa serikali yake mapema kwa kuiagiza TRA iwajibike ipasavyo katika kukusanya mapato, lakini mapato hayo yasiwe ya dhuluma. Rais Dk. Samia anataka kila mwananchi mwenye sifa za kulipa kodi alipe.

Aprili 6, 2021, Rais Dk. Samia alipokuwa akiwaapisha makatibu wakuu na manaibu wao, alitoa maelekezo mahsusi kwa TRA. "Kukusanya kodi kwa mabavu havisaidii kwa muda mrefu. Nimepewa takwimu ya zile taskforce (vikosikazi vya kukusanya kodi) mlizoziunda lakini havisaidii, mnawatisha watu wanalazimika kufunga biashara."

"Tunazitaka kodi lakini kodi za dhuluma hapana. Kwa sababu hazitatufikisha mbali. Jinsi ya kurudisha wafanyabiashara, kutengeneza wigo wa kukusanya kodi, nafahamu uamuzi huu niliochukua tutayumba kwa miezi miwili, mitatu lakini baada ya muda tutarudi vizuri," amesema Rais Dk. Samia.

Msisitizo wa kuongeza mapato ulitokana na ukweli kuwa mipango mingi na mizuri aliyonayo Rais Dk. Samia kwa wananchi wake, haitaweza kufanikiwa kama TRA haitakusanya kodi kikamilifu ambayo ndiyo kichochea cha kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Awali, TRA ilikuwa na utaratibu wa kufunga biashara na shughuli mbalimbali pale ambapo mlipakodi atashindwa kulipa kodi kwa wakati. 

Vilevile, katika makadirio ya kodi, baadhi ya wafanyabiashara walikuwa wakilalamikia kuwekewa makadirio makubwa tofauti na kiwango cha biashara zao. Hii iliweka uadui mkubwa kati ya TRA na walipakodi nchini.

MAGEUZI MAKUBWA YAMEONDOA UADUI KATI YA TRA NA WALIPAKODI

Kutokana na maelekezo ya Rais. Dk. Samia kwa TRA, uadui uliokuwepo awali kati ya TRA na walipakodi umeondoka. Hii inatokana na mtazamo chanya alioujenga Rais Dk. Samia kwa pande zote mbili. 

Kimsingi, pande zote mbili zinategemeana. TRA anamtegemea mlipakodi kwani pindi kodi inapolipwa ndipo inawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo inamnufaisha mlipakodi moja kwa moj.

Rais Dk. Samia akasisitiza pawepo na meza ya mazungumzo na makubaliano ya namna gani mlipakodi atalipa kodi pale ambapo atashindwa kulipa kwa wakati.

Aidha, Rais Samia akasisitiza kuwa kufunga biashara ni kummaliza kabisa mlipakodi kwani biashara yake itakapofungwa, ndipo atashindwa kabisa kulipa kodi kwani hatakuwa na shughuli ya kumuingizia kipato cha kuwezesha kulipa kodi na wala TRA haitaweza kupata kodi yake.

Kongole kwa Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, pamoja na wasaidizi wake nchi nzima wamefanyia kazi maelekezo ya Rais, na sasa tunashuhudia mafanikio ya kumalizika kwa uadui uliokuwepo awali.

Ni faraja kuona tunapoadhimisha miaka 30 ya TRA, kumejengeka uhusiano mzuri kati ya mlipakodi na mamlaka. Hakuna mabavu wala ubabe. Uhusiano mzuri uliopo umewezesha kuongezeka kwa mapato ya serikali.

Mathalani, mwezi Machi, 2026,  TRA wamefanikiwa kukusanya trilioni 3.58, na kimsingi, ongezeko la makusanyo yamewezesha hata bajeti ya mwaka 2026/2027, kutegemea mapato ya ndani kwa asilimia 74.2.

Maoni : 0620 800 462
Posted by MROKI On Wednesday, June 24, 2026 No comments

June 23, 2026






Na Benny Mwaipaja, Dodoma
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, limepitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

Akitangaza matokeo ya kura ya wazi iliyopigwa bungeni jijini Dodoma, Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azzan Zungu alisema kuwa kati ya kura hizo 393 zilizopigwa, kura 8 zimekataa kuunga mkono bajeti hiyo na wabunge wengine nane 8 hawakupiga kura kwa sababu hawakuwepo bungeni.

Akihitimisha hoja baada ya Bunge kupitisha Muswada wa Sheria kwa ajili ya kuidhinisha Serikali kuanza kutekeleza Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/2026 (zaidi ya shilingi trlilioni 62.33) kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina, Mhe. Spika Zungu alimpongeza Waziri wa Fedha, Mhe. Ballozi Khamis Mussa Omar (Mb) wasaidizi wake, watendaji wa Wizara kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya na Wabunge wote kwa michango yao yenye tija kwa Taifa.

“Kura zimepigwa na Serikali imeruhusiwa kuzitumia pesa kuanzia sasa, mkazitumie pesa hizi kama Kamati za Bunge zilivyoelekeza, kuhakikisha maslahi ya watu kwanza yanazingatiwa kabla ya mambo mengine. Bunge hili litaendelea kufuatilia utekelezaji wake na kuhakikisha kuwa miradi yote iliyoainishwa inazingatiwa na kuleta furaha kwa wananchi” alisisitiza Mhe. Zungu.

Kupitia kwa Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), Serikali ililiomba Bunge lipitishe Bajeti ya shilingi trilioni 62.33 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo katika Mwaka wa Fedha 2026/2027, ikiwa ni ongezeko la asilimia 10.3 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2025/26. 

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, mapato yalitarajiwa kuwa shilingi trilioni 46.79 ambapo mapato ya kodi ni shilingi trilioni 36.99, mapato mengine ni shilingi trilioni 9.24 (ikijumuisha mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa shilingi trilioni 1.977) na misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo shilingi bilioni 563.1.

Aidha aliongeza kuwa ili kuendana na dhamira ya kujitegemea katika uendeshaji wa Serikali na maendeleo, takribani robo tatu ya bajeti yote ya mwaka 2026/27, sawa na asilimia 74.2 itagharamiwa na mapato ya ndani.

Matumizi na uwekezaji katika mali zisizo za kifedha yalikadiriwa kuwa shilingi trilioni 54.50 pasipo kujumuisha malipo ya mtaji wa deni la Serikali ambapo kati ya kiasi hicho, stahiki za watumishi ikijumuisha michango ya pensheni ni shilingi trilioni 10.13.

“Gharama za bidhaa na huduma itakuwa shilingi trilioni 5.22, malipo ya riba ni shilingi trilioni 6.86, ruzuku shilingi trilioni 25.32, mafao na misaada ya kijamii shilingi trilioni 1.01, uwekezaji katika mali zisizo za kifedha shilingi trilioni 2.33 na gharama nyingine shilingi trilioni 3.63.” alisema Mhe. Balozi Omar

Aliongeza kuwa kulingana na makadirio ya mapato na matumizi hayo, kunajitokeza nakisi kwenye bajeti ya shilingi trilioni 7.71 na Serikali itaendelea kugharamia nakisi ya bajeti hiyo kwa kutumia mikopo kutoka vyanzo vya ndani na nje kwa kuzingatia Mkakati wa Muda wa Kati wa Kusimamia Deni la Serikali (2025/26 – 2027/28).

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, katika mwaka 2026/27, Serikali inatarajia kukopa jumla ya shilingi trilioni 15.54 ambapo kati ya kiasi hicho, mikopo ya ndani itakuwa shilingi trilioni 6.56, mikopo ya nje yenye masharti nafuu shilingi trilioni 6.55 na mikopo ya nje yenye masharti ya kibiashara shilingi trilioni 2.43.
Aidha, Serikali inakadiria kulipa malipo ya mtaji kwa mikopo iliyoiva shilingi trilioni 7.84.

Baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo, Bunge linatarajia kupokea, kujadili na kupitisha Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2026 ( The Finance Bill,2026) tarehe 24 Juni, 2026.

Mwisho
 
 
Captions

PIX : 1

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, akimpongeza Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX:2

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na Naibu Mawaziri wake, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) na Mhe. Laurent Luswetula (Mb) wakipongezwa na Wabunge mbalimbali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, baada ya wabunge hao kupitisha kwa kishindo makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali ya shilingi Trilioni 62.33 kwa mwaka 2026/2027, ambapo zaidi ya wabunge 385 sawa na asilimia 97.66 walipitisha kwa kura za ndio.

PIX:3

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, wakipongezana baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX:4

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akipongezwa na Wafanyakazi wa Shule ya Awali na Msingi ya Mzigu ya mkoani Mwanza, baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX: 5

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi waandamizi wa Wizara ya Fedha na Wizara ya Mipango na Uwekezaji, baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX:6

Manaibu Katibu Wakuu wa Wizara ya Fedha, Bw. Elijah Mwandumbya (kushoto) na Bw. Joshua Nsubili, wakipongezana baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)
Posted by MROKI On Tuesday, June 23, 2026 No comments

June 22, 2026







Dodoma
Banda la Tume ya Madini limeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa mamia ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, huku wengi wakijitokeza kupata elimu kuhusu sekta ya madini, huduma zinazotolewa na Tume  pamoja na fursa zilizopo katika shughuli za utafutaji, uchimbaji na biashara ya madini.

Miongoni mwa waliotembelea banda hilo ni Lusajo Luena kutoka Dodoma, ambaye amesema elimu aliyoipata imemwezesha kuelewa taratibu za upatikanaji wa leseni za madini na wajibu wa wamiliki wa leseni katika kuendeleza maeneo yao ya uchimbaji.

"Kabla ya kufika hapa sikuwa na uelewa wa kina kuhusu namna leseni za madini zinavyotolewa na kusimamiwa. Leo nimepata elimu ya kutosha kuhusu taratibu mbalimbali na umuhimu wa kuzingatia sheria za madini," amesema Luena.

Kwa upande wake, Joyce Kitundu kutoka Dodoma amesema maelezo aliyopata katika banda hilo yamemsaidia kufahamu mchango mkubwa wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa taifa na namna Serikali inavyosimamia rasilimali za madini kwa manufaa ya wananchi.

"Nimejifunza kuwa sekta ya madini ni nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi. Pia nimeelewa majukumu ya Tume ya Madini katika kusimamia shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini," amesema Kitundu.

Naye Glory Daudi kutoka Kondoa amesema elimu aliyopata imefungua fursa mpya za uelewa kuhusu ushiriki wa vijana na wanawake katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na sekta ya madini.

"Nimefurahishwa na elimu niliyopewa kuhusu fursa zilizopo kwenye sekta ya madini. Sasa nimeelewa kuwa si lazima mtu awe mchimbaji pekee, kwani kuna fursa nyingi za biashara na utoaji huduma zinazozunguka sekta hii," amesema Daudi.

Tume ya Madini inaendelea kutumia maonesho hayo kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali zinazotolewa pamoja na kuhamasisha ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.
Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments
Na Adelina Johnbosco - MAELEZO
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara, ameipongeza Ofisi ya Msemaji Mkuu wa Serikali na kusema inafanya kazi kubwa ya kuzitangaza shughuli zinazotekelezwa na Serikali pamoja na kuwafikia wananchi.

Prof. Kahyarara amesema hayo Juni 22, 2026, alipotembelea banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na taasisi zake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kwenye viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.

"Serikali ina shughuli nyingi zinazofanyika ikiwemo miradi mbalimbali, mipango na malengo kwa ajili ya maendeleo na maslahi ya wananchi, hata ukisema kila siku au kila wiki utoke na kitu kimoja lakini bado inakuwa haitoshi, lakini Ofisi ya Msemaji Mkuu wa Serikali inajitahidi kwa kufanya kazi kubwa kwani taarifa zinatolewa kuhusu yanayotekelezwa na Serikali kwa wananchi wake" ameongeza Prof. Kahyarara.

Kwa upande mwingine, ameipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kufikia hatua nzuri katika maandalizi ya AFCON 2027 pia na taifa kwa ujumla kuwa miongoni mwa nchi zilizochaguliwa kuwa mwenyeji wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) yanayotarajiwa kufanyika nchini Tanzania mwaka 2027.

"Hii inaonesha jinsi gani Tanzania imefikia hatua ya juu katika michezo na imeaminika na ina uwezo wa kuhudumia wageni, lakini pia itakuwa fursa ya kuutangaza utamaduni wetu kwa mataifa mengine" - Prof. Kahyarara. 

Aidha, amesema Wizara ya Uchukuzi tayari imejipanga katika sekta zake za usafiri na usafirishaji kwa kuhakikisha inawahudumia wenyeji na wageni kabla, wakati na baadaya ya AFCON 2027.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026 na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi. Dkt.  Moses Kusiluka
Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments
Afisa Usimamizi wa Fedha Mkuu, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Abdul Dachi, akitoa elimu kwa wananchi wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Afisa Habari Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Eva Valeria (kulia) na Afisa Habari, Wizara ya Fedha, Bw. Joseph Mahumi, wakimpa mwanafunzi wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP), Bi. Nice Justace, maelekezo wa namna ya kujiunga na mitandao ya kijamii ya Wizara ya Fedha, ikiwemo, Instagram (urt mof), Facebook (Wizara ya Fedha), LinkedIn (Ministry of Finance -Tanzania), Youtube – Hazina TV.
Afisa Usimamizi wa Fedha Mwandamizi, Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Bi. Grace Samwel, akitoa elimu kwa wanafunzi wa Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) kuhusu matumizi ya huduma rasmi za kifedha, walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Mchumi Daraja la Kwanza, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPU), Wizara ya Fedha, Bi. Anastazia Amandi, akitoa elimu kwa mwananchi kuhusu mafanikio ya Ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP), walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, kuhusu majukumu yanayotekelezwa na wizara hiyo, wakati wananchi hao walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kauli mbiu ‘Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Maendeleo Endelevu’, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, kuhusu majukumu yanayotekelezwa na wizara hiyo, wakati wananchi hao walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kauli mbiu ‘Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Maendeleo Endelevu’, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Na Saidina Msangi na Asia Singano, WF - Dodoma
Wizara ya Fedha imeendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhakikisha wananchi wanapata ufafanuzi kuhusu masuala ya kodi, uchumi na sera mbalimbali za fedha na mchango wa kodi katika kugharamia huduma muhimu za kijamii kama vile miundombinu, elimu, afya, maji nishati na huduma nyingine muhimu.
 
Hayo yamebainishwa na Afisa Usimamizi wa Fedha Mkuu, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Abdul Dachi, wakati akitoa elimu kwa wananchi kwenye  Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
 
Bw. Dachi alisema kupitia Maonesho hayo, Idara imekuwa ikitoa taarifa kwa wananchi kwa lugha rahisi na inayoeleweka ili kuwawezesha kufahamu mchango wa Sera za Kodi na Uchumi katika maendeleo ya Taifa na ustawi wa jamii.
 
‘‘Miongoni mwa maeneo yanayotolewa elimu ni kuhusu mwenendo wa uchumi wa Taifa na namna Sera za Uchumi zinavyosaidia kudhibiti mfumuko wa bei, kuongeza fursa za ajira na kukuza uchumi kwa ujumla pamoja na namna hizo zinavyoandaliwa ili kuhakikisha mapato ya Serikali yanakusanywa kwa ufanisi na kwa kuzingatia maslahi ya Taifa,’’, alisema Bw. Dachi.
 
Aliongeza kuwa Serikali inatumia taarifa za takwimu na tafiti mbalimbali zinazosaidia katika upangaji wa bajeti na utekelezaji wa mikakati ya maendeleo ya muda mfupi na mrefu pamoja na usimamizi wa mikataba ya kikodi kati ya Tanzania na mataifa mengine na ushirikiano wa kikanda na kimataifa unaolenga kulinda maslahi ya Taifa katika sekta ya kodi.
 
Alifafanua kuwa wananchi wanapatiwa elimu kuhusu namna Wizara inavyofanya tafiti za kisera na kuandaa mapendekezo ya kitaalamu yanayosaidia Serikali kufanya maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya nchi pamoja na namna Serikali inavyoshughulikia masuala ya kodi za kimataifa.
 
‘’Tumetumia fursa hii kueleza wananchi umuhimu wa sera za kodi na fedha katika kukuza uchumi na ustawi wa wananchi, mchango wa kodi katika maendeleo ya Taifa, pamoja na umuhimu wa uwazi na uwajibikaji katika mchakato wa utungaji wa sera nafasi ya Tanzania katika uchumi wa dunia na manufaa yanayotokana na ushirikiano wa kiuchumi na mataifa na taasisi mbalimbali za kimataifa’’, alifafanua Bw. Dachi.
 
Alisema kuwa ili kuhakikisha ujumbe unawafikia wananchi wengi zaidi, idara pia inatoa vipeperushi, vitabu vya elimu pamoja na mazungumzo ya ana kwa ana na wageni wanaotembelea Banda hatua inayochangia kuongeza uelewa wa umma na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na wananchi katika maendeleo ya Taifa.

Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments

June 21, 2026





📍Dodoma
Tume ya Madini imeendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa leseni za madini nchini kwa lengo la kufuatilia maendeleo ya leseni hizo na kuhakikisha shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini zinafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Akizungumza katika Banda la Tume ya Madini kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park mkoani Dodoma, Mtakwimu kutoka Kurugenzi ya Leseni ya Tume ya Madini, Azihar Kashakara, amesema ukaguzi huo ni muhimu katika kuhakikisha wamiliki wa leseni wanatimiza masharti na wajibu unaotokana na leseni walizopewa.

Amesema kuwa, pamoja na kufuatilia maendeleo ya leseni, Kurugenzi ya Leseni ina jukumu la kutoa na kusimamia leseni za madini, kutafsiri na kusambaza takwimu za leseni, pamoja na kuwezesha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali yatokanayo na umiliki wa leseni hizo.

Kashakara ameeleza kuwa utoaji wa leseni za madini unazingatia masharti na vigezo vilivyowekwa kisheria, hivyo waombaji wanapaswa kuyatimiza ili kuwezesha upatikanaji wa leseni kwa wakati. 

Aidha, ametoa ufafanuzi kuhusu ada na tozo mbalimbali zinazohusiana na leseni za madini, sambamba na kueleza tofauti kati ya umiliki wa ardhi (Surface Rights) na umiliki wa haki za madini (Mineral Rights).

Tume ya Madini ni miongoni mwa taasisi zinazoshiriki Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma chini ya kaulimbiu isemayo, “Kuchochea Uwajibikaji kwa Huduma Endelevu.” 

Kupitia maonesho hayo, wananchi na wadau wa sekta ya madini wanapata fursa ya kuelimishwa kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na Tume ya Madini pamoja na mchango wake katika usimamizi endelevu wa rasilimali za madini kwa maendeleo ya taifa.
Posted by MROKI On Sunday, June 21, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo