Nafasi Ya Matangazo

December 05, 2025









Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi amezindua rasmi mita janja (smart meter) yenye lengo la kuboresha na kumrahisishia mteja kufanya manunuzi ya umeme moja kwa moja  ikiwa ni mageuzi makubwa ya teknolojia  yanayofanywa na TANESCO katika kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wateja.

Waziri wa Nishati amezindua Mita janja hizo Disemba 05, 2025 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), na kuhudhuriwa na viongozi  mbalimbali wa Serikali, wadau wa sekta ya nishati na watendaji wa TANESCO.

Amesema Mita hizo mpya zinamwezesha mteja kupata umeme mara moja baada ya kufanya manunuzi ya token bila kutumia kifaa cha ziada cha kuingiza namba (CIU), hatua inayolenga kupunguza changamoto zilizokuwa zikijitokeza katika mfumo wa zamani.

“Leo tunajivunia hatua kubwa ya  kihistoria zilifanywa na TANESCO ikiwa ni  moja ya kampuni za umma inayofanya vizuri katika utoaji huduma kwa wateja nchini. Mita janja inaleta mapinduzi makubwa katika namna Shirika hili linavyofanya usimamizi wa ukusanyaji wa mapato,” ameeleza Mhe. Ndejembi.

Ameongeza kuwa changamoto zilizokuwa zikiwakabili wateja wakati wa kuingiza token ndiyo zimeisukuma Serikali kufanya mageuzi  ya kiteknolojia.

“Uzinduzi huu unaweka alama kubwa  kwa nchi yetu kwenye mapinduzi ya tekinolojia ,  hivyo naielekeza TANESCO kuhakikisha inasamabaza mita hizi maeneo yote yenye uhitaji mkuwa na kuhakikisha inaendana na viwango vya kimataifa sambamba na kutoa elimu za faida ya mita hizo,” alisisitiza. 


Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema uzinduzi wa Mita Janja ni mwendelezo wa dhamira ya Serikali katika kuboresha huduma kwa wananchi.

“Nimefurahi kushuhudia hatua hii kubwa ya mapinduzi, ikiwa ni siku ya 33 tangu Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aingie madarakani. Leo tunaweka historia muhimu kupitia uzinduzi wa Mita Janja kwa wateja wa TANESCO,” alisema Mhe. Salome.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, amesisitiza umuhimu wa kulinda miundombinu ya umeme na kupongeza TANESCO kwa kuimarisha ushirikiano na vyombo vya ulinzi na usalama katika kudhibiti vitendo vya uharibifu.

“Hatua hii itukumbushe wajibu mkubwa tulionao kulinda miundombinu. Nawapongeza TANESCO kwa ushirikiano wao na Jeshi la Polisi katika kupambana na uhujumu dhidi ya miundombinu. Endeleeni kwa kasi hii ili huduma ya umeme ipatikane kwa uhakika,” alisema , Mhe. Chalamila.

Aidha, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mha. Felichesmi Mramba, ametoa pongezi kwa TANESCO kwa utekelezaji huu kwa wakati muafaka, akieleza kuwa teknolojia ya Mita Janja itarahisisha kwa kiwango kikubwa utambuzi wa changamoto za wateja kabla ya mteja kutoa taarifa TANESCO.

Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TANESCO, Balozi Zuhura Bundala, alisema Bodi inaona fahari kuona mageuzi yanayoendelea katika uboreshaji wa huduma zinazotolewa na Shirika na kuwa bodi hiyo inazidi kupata moyo katika kuliongoza Shirika kutoa huduma bora zaidi kidigitali.
Posted by MROKI On Friday, December 05, 2025 No comments



WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Rais wa vitendo na amethibitisha hayo katika kipindi alichoingoza Tanzania kwa kuboresha miundombinu kwenye sekta mbalimbali.

Amesema mafanikio makubwa yamepatikana chini ya uongozi wake wa miaka minne na nusu ikiwemo ujenzi wa hospitali 119 katika wilaya zisizo na hospitali, vituo vya afya 640 katika kata za kimkakati na tarafa, zahanati zaidi ya 800 vijijini pamoja na ujenzi wa shule mpya za msingi zaidi ya 2,700.

“Amejenga shule za sekondari zaidi ya 1,300 na madarasa 79,000 katika maeneo yaliyokuwa na uhitaji wa madarasa. Haya yamesaidia kuondoa tatizo la wanafunzi kusubiri kujiunga na sekondari kwa sababu ya uhaba wa madarasa. Hatua hii imemaliza utaratibu wa uchangishwaji kwa nguvu na kamatakamata za ujenzi wa vyumba vya madarasa,” amesema.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Desemba 05, 2025) wakati akizungumza na maelfu ya wakazi wa Ilemela na Nyamagana katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Nyamagana, jijini Mwanza.

Akielezea kuhusu utendaji kazi wa Rais, Waziri Mkuu amesema ujenzi wa miundombinu bora ya elimu na afya iliyojengwa na Serikali, inahitaji watumishi wa kutosha na ndiyo maana Rais ametoa msukumo wa haraka kwenye ajira hizo na ndiyo maana aliahidi maeneo 13 ya vipaumbele ndani ya siku 100 tangu ashike madaraka.

Dkt. Mwigulu amesema ili kutekeleza ahadi za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia, Serikali imeidhinisha ajira mpya 12,000 zikijumuisha 5,000 za kada ya afya na 7,000 za sekta ya elimu ambapo usaili utaanza Desemba 10, 2025 katika kila mkoa na watumishi hao wataanza kuripoti vituoni kuanzia Januari 10, 2026 hatua ambayo itaimarisha zaidi utoaji wa huduma nchini. “Nia ya Serikali ni kufanya vituo vya afya na shule zetu zipate watumishi,” amesisitiza.

Amesema kuwa Rais Samia ametekeleza mambo makubwa katika maboresho ya mifumo ya kijamii ikiwemo kuanza utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote ambapo makundi ya watoto, wazee na wajawazito ndiyo yatakuwa ya kwanza kunufaika. 

Kabla ya mkutano huo, Waziri Mkuu alikagua uharibifu uliofanywa wakati wa vurugu za Oktoba 29, mwaka huu kwenye kata za Kisesa, Buzurugwa na Nyasaka ambako alioneshwa ofisi za watendaji na mali za watu binafsi zilizochomwa moto. Pia alitembelea kiwanda cha magodoro cha Banco na kuelezwa uharibifu wa mali uliofanyika.

Amewataka Watanzania wasikubali kuyumbishwa na watu wasioitakia mema Tanzania. “Kila Mtanzania anaowajibu wa kuipenda Tanzania, tusiyumbishwe na watu wasiotutakia mema, Tanzania ni ya Watanzania tuijenge na tuilinde nchi yetu. Akitokea mtu anakwambia uharibu mali ya umma, ujue huyo ana nia ya kuihujumu Tanzania, mkatalieni.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemuagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa amsake mwalimu anayetuhumiwa kumbaka binti wa Mama Florah Anthony, mkazi wa Nyasaka ambaye alifikisha kilio chake mbele ya Dkt. Mwigulu. 

"RPC chukua hatua, nataka nione mwisho wa suala hili. Tuma vijana wako, huyu mtuhumiwa akamatwe, uchunguzi ufanyike na ikithibitika ana hatia afunguliwe kesi ya ubakaji."

Mkuu wa Mkoa, fuatilia suala hili. Ikithibitika ametenda hilo kosa, afukuzwe kazi. Nasema afukuzwe na siyo ahamishiwe kwenye kituo kingine," amesisitiza.
Posted by MROKI On Friday, December 05, 2025 No comments

December 03, 2025




WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Watanzania wanataka kuiona nchi yao ikifikisha lengo la uchumi wa kati wa dola za Marekani trilioni moja ifikapo mwaka 2050 na watakaofanikisha jambo hilo ni sekta binafsi ikiwemo wenye wabunifu kutoka kwenye kampuni changa.

“Mtakumbuka kuwa Julai, mwaka huu Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alizindua DIRA 2050. Dira hii si ya Serikali peke yake bali ni kielelezo cha matarajio ya Watanzania ambao wanataka nchi yao ifikie uchumi wa kati wa dola za Marekani trilioni moja ifikapo mwaka 2050. Injini ya kuendesha nchi kuelekea maono haya ni sekta binafsi zikiwemo kampuni changa zinazoanzishwa,” amesema.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumatano, Desemba 03, 2025) wakati akifunga maadhimisho ya Wiki ya Kampuni Changa za Teknolojia (start-ups) kwenye ukumbi wa PSSSF, Makumbusho, jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu ambaye alikuwa akimwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema kazi ya kufikisha lengo siyo ndogo na inahitaji mabadiliko ya kiutendaji na kimtazamo. “Hatuwezi kufikia uchumi wa dola trilioni moja kwa kuendelea kuuza bidhaa ghafi au kufanya mabadiliko kidogo tu. Inatutaka tuwe na mbinu bunifu zenye tija: tuwe na njia mipya za kufanya mambo, tuanzishe makampuni mapya, tuwe na bidhaa mpya na teknolojia mpya zinazoweza kukua mara 10 badala ya asilimia 10.”

“Inahitaji tuje na ubunifu wa Kitanzania utakaovutia mataifa na kuzalisha masoko ya nje. Inawezekana kabisa, twendeni tuunganishe nguvu,” amesisitiza.

Amesema vijana waliochukua hatua ya kuanzisha kampuni changa wao ndiyo wenye hatma ya Tanzania na kwambo njia hiyo ndiyo sahihi ya kutenda kwa njia mbadala. “Nchi nyingi za Afrika zinakabiliwa na changamoto ya vijana kutojiamini. Lakini wapo wengi ambao wametoa ajira kwa vijana wenzao. Na hii ndiyo njia sahihi ya kufanya mambo kwa njia mbadala kama ambavyo wenzeyu wamefanya.”

Amewataka Watanzania waiheshimu sekta binafsi kama wanavyoiheshimu sekta ya umma kwa kuanza kubadilisha mtazamo wao ikiwemo nidhamu ya utendaji kazi. “Kwa mazingira ya sasa, hakuna nchi imeweza kujenga uchumi mkubwa bila kuishirikisha sekta binafsi. Hiki mnachokifanya ndiyo injini ya kukuza uchumi,” amesema.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa maadhimisho hayo, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Anjela Kairuki alisema Seriklai imeendele akuboresha mazingira ya kampuni changa ambapo hadi sasa kampuni changa za Kitanzania zinakadiriwa kufikia 1,041 na kuzalisha ajira zaidi ya 140,000.

Alisema hadi kufikia mwaka 2024, kampuni hizo zilikuwa zimeingiza mapato ya dola za marekani milioni 96.4 na kwamba hadi kufikia sasa zimekwishafikisha mapato ya dola za Marekani milioni 300.

Alisema kampuni nyingi zinazochipukia zimejielekeza kwenye matumizi ya teknolojia za huduma za kifedha, kilimo, afya, elimu na kwamba bado wanatarajia kuwa na bunifu nyingi za kidijitali. 
Posted by MROKI On Wednesday, December 03, 2025 No comments

December 01, 2025



Na Mwandishi Wetu-Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. William V. Lukuvi, amewahakikishia Watanzania kuwa dawa za kufubaza makali ya Virusi vya UKIMWI (ARVs) zinapatikana kwa asilimia 100 nchini na zinatolewa bila malipo kwa watu wote wanaoishi na VVU (WAVIU).
 
Amesema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akitoa Tamko la Serikali kuhusu Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani ambapo kwa mwaka 2025 yamefanyika chini ya kaulimbiu: “Imarisha Mwitikio, Tokomeza UKIMWI”.
 
Waziri Lukuvi amesema upatikanaji wa dawa hizo umeendelea kuimarika, huku idadi ya WAVIU wanaotumia Dawa za ARV ikiongezeka kutoka asilimia 98 mwaka 2024 hadi asilimia 98.5 mwaka 2025, hatua inayochochea kupungua kwa athari za UKIMWI na kuboresha afya za wananchi.
 
Aidha, Waziri Lukuvi amebainisha kuwa Serikali imeongeza idadi ya vituo vinavyotoa huduma za tiba na matunzo kwa WAVIU ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za VVU na UKIMWI nchini. Vituo hivyo vimeongezeka kutoka vituo 7,805 mwaka 2024 hadi vituo 8,203 mwaka 2025.
 
Ameongeza kuwa, huduma za ufuatiliaji wa matibabu kwa WAVIU zinaendelea kuimarishwa, huku serikali ikiboresha upatikanaji wa huduma za maabara kwa kuongeza mashine za kupima wingi wa VVU mwilini. Kwa sasa, zipo mashine kubwa 50 kutoka 43 mwaka 2024, na mashine ndogo 127, hivyo kufanya kuwa na jumla ya mashine 177 zinazoendelea kutoa huduma nchini.
 
Katika tamko lake, Waziri Lukuvi amesisitiza kuwa Siku ya UKIMWI Duniani ni muhimu kwa kutathmini hali na mwelekeo wa kudhibiti VVU na UKIMWI nchini na kimataifa, kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya maambukizi mapya, kuwakumbuka waliopoteza maisha kutokana na ugonjwa wa UKIMWI, na kuwaenzi watu wanaoishi na VVU pamoja na yatima wanaotokana na athari za UKIMWI.
 
Amesema Serikali inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha kuwa ajenda ya kudhibiti UKIMWI inaendelea kupewa kipaumbele katika ngazi zote za uongozi na utungaji sera.
Posted by MROKI On Monday, December 01, 2025 No comments

November 30, 2025




WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Novemba 30, 2025, amekagua Mahakama ya Mwanzo iliyopo Maji ya Chai ambayo iliharibiwa kutokana na vurugu zilizotokea Oktoba 29, 2025, mkoani Arusha.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu yupo mkoani Arusha kwa ziara ya kukagua uharibifu uliojitokeza kufuatia vurugu za Oktoba 29, 2025.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ameambatana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Amosi Makalla.





WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Novemba 30, 2025, amekagua Kituo cha Mafuta cha Total kilichopo Maji ya Chai ambacho kiliharibiwa kutokana na vurugu zilizotokea Oktoba 29, 2025, mkoani Arusha.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu yupo mkoani Arusha kwa ziara ya kukagua uharibifu uliojitokeza kufuatia vurugu za Oktoba 29, 2025.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ameambatana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Amosi Makalla.
Posted by MROKI On Sunday, November 30, 2025 No comments


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameliagiza Jeshi la Polisi liache kumtafuta Askofu Dkt. Josephat Gwajima kama walivyokuwa wametangaza awali ili aweze kuendelea shughuli zake.

Amesema baada ya kutoa msamaha kwa Kanisa la Ufufuo na Uzima, waumini wanahitaji wamuone kiongozi wao, hivyo anatakiwa ajitokeze hadharani aendelee na kazi yake. “Mwacheni ajitokekeze tujenge umoja wa kitaifa, tushikamane kurudisha umoja wa kitaifa. Tumekutana na TEC, viongozi wa dini, wa mila na viongozi mbalimbali; twendeni sote kwenye jambo hili, tujitokeze tuhamasishe Tanzania yenye amani, huu ndio wito wa kiongozi wetu wa nchi”

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumapili, Novemba 30, 2025) wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa Arumeru katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Magufuli Leganga, kata ya Usa River, wilayani Arumeru mkoani Arusha.

Waziri Mkuu amewataka Watanzania wakatae kushawishiwa na wanaharakati wanaochochea vurugu kwani zinarudisha nyuma maendeleo ya nchi. "Nimekuja kuwapa pole wananchi wenzangu, kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Anatambua mambo yanayoendelea. Anatambua kazi kubwa ya kujenga Taifa mnayoifanya," amesema.

Kabla ya mkutano huo, Waziri Mkuu alikagua uharibifu uliofanywa wakati wa vurugu za Oktoba 29, mwaka huu kwenye kituo cha polisi cha Kikatiti (mita 500 kutoka barabara kuu ya Arusha - Moshi); Mahakama ya Mwanzo ya Maji ya Chai (km. 3 kutoka barabara hiyo kuu); kituo cha mafuta Total Energies kilichopo Maji ya Chai (kipo barabarani) ambavyo vyote vilichomwa moto ikiwemo kuiba mali kwenye supermarket na kubomoa sefu ya kutunzia fedha.

Waziri Mkuu amesema masuala ya maendeleo ya wilaya ya hiyo kama vile maji na barabara yamo kwenye Ilani ya CCM na kwenye ahadi za Mheshimiwa Rais lakini yatafanyika endapo tu nchi itakuwa na amani. “Tukichagua vurugu tutakuwa tumechagua kufukuza maendeleo, tukichagua vurugu tutakuwa tumechagua kuongeza umaskini kwa mtu mmoja mmoja," ameonya.

"Kila Mtanzania akatae haya yaliyotokea juzijuzi. Tumechochewa, tumechonganishwa lakini wao wako nje, wanalipwa ili kutuvuruga tu. Wengi wanaochochea vurugu ni wanaharakati, wako nje ya nchi. Hakuna kiongozi wa chama cha siasa anasema wananchi wafanye vurugu. Au mmemuona?" alihoji.

Amesema baadhi ya vijana walioko nje ya nchi wamebainika kupokea dola za Marekani milioni mbili (sawa na sh. bilioni 4.5) ili wachochee vurugu. “Hawa wanaowalipa, wana maslahi gani na nchi yetu? Wana ajenda gani na nchi yetu? Tunajua watazirudishaje hizo fedha?”

“Hawa watu wanalenga tugombane ili wachukue madini adimu (rare earth minerals). Sasa hivi Tanzania imegundua uranium ambapo inakuwa nchi ya tisa duniani na ya kwanza barani Afrika. Ina tani za ujazo 890,000. Hii ni karibu tani milioni moja."
 
Waziri Mkuu ameonya dhidi ya mchezo unaotumika kuanzisha chokochoko ili kusambaratisha nchi pindi inapobainika kuwa na rasilimali. Amesema ziko baadhi ya nchi barani Afrika ziliathirika kutoka na chokochoko hizo. “Wanaanzisha chokochoko, wanaacha mnavurugana, rasilmali zikiisha, wao wanaondoka,” amesisitiza.

"Watanzania tuamkeni, tuchukue tahadhari. Kuna kamchezo kanachezwa. Wanajua Tanzania ina gesi asilia nyingi na inakaribia kuanza. Wanajua ikianza miradi hii, Tanzania itakuwa ya kwanza katika Afrika Mashariki na wala hatutahitaji kutoa mikopo ya wanafunzi."

Amewataka Watanzania waamke na kukataa kurudishwa tena kwenye hali ya vurugu. "Watanzania tuamke, tukatae kurejeshwa kule nyuma. Umaskini utaondolewa nchi ikiwa kwenye amani. Ajira za vijana zitaweza kupatikana nchi ikiwa kwenye amani."

Amesisitiza kuwa vurugu zikiwepo, hata wakulima wa karoti na nyanya wa Ngarenanyuki hazitauzwa na hivyo kuathiri uchumi wa mtu binafsi.
Posted by MROKI On Sunday, November 30, 2025 No comments

November 29, 2025









Na Mwandishi Wetu, Nyang'wale, Geita
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde akiwa ziarani Wilayani Nyang'wale amewaasa na kuwataka wamiliki wa leseni za uchimbaji wa madini kuzingatia Sheria ya Madini Sura ya 123 na Kanuni zake katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akizungumza katika ziara hiyo iliyofanyika kwenye eneo la mgodi wa Kasubuya wilayani Nyang’hwale, Waziri Mavunde amesema wachimbaji wadogo kwa sasa wanachangia zaidi ya asilimia 40 ya mapato yatokanayo na sekta ya madini, akibainisha kuwa mchango wao unaendelea kuongezeka kutokana na maboresho makubwa ya Sheria, Kisera na Kiutendaji yanayofanywa na Serikali.

Waziri Mavunde aliongeza kuwa kufuatia mabadiliko ya Sheria ya mwaka 2024, kuanzia Oktoba 1, 2024, Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ilianza ununuzi rasmi wa dhahabu nchini na kufanikiwa kununua zaidi ya tani 15 hadi sasa. Hatua hiyo imeiwezesha Tanzania kuingia kwenye orodha ya nchi 10 bora barani Afrika zinazomiliki hifadhi kubwa ya dhahabu.

Akiwahimiza wachimbaji na wamiliki wa Leseni kuzingatia Sheria, Waziri Mavunde amesisitiza kuwa leseni za uchimbaji hazipaswi kupangishwa wala kuachwa bila kuendelezwa na kutaka wamiliki wa Leseni kuzingatia kanuni mpya zinazohitaji kuingia makubaliano na wamiliki wa maduara na kuyasajili makubaliano hayo ofisi ya Tume ya Madini.

“Mtu yoyote ambaye amepewa leseni anatakiwa aiendeleze. Hakuna kuhodhi eneo bila shughuli za maendeleo. Leseni zote zisizoendelezwa, nataka niwahakakikishie ninakwenda kuzifuta mara moja ili wapewe wengine wenye uwezo wa kuziendeleza” amesema.

Katika kuboresha huduma za uchunguzi wa madini, Mavunde ametangaza kuwa Serikali inajenga maabara tatu kubwa katika mikoa ya Geita, Dodoma na Chunya ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wachimbaji.

Amesema pia, Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameagiza kufanyika kwa Utafiti wa kina wa madinini ambapo kwasasa Wizara inajipanga kutekeleza mradi wa ununuzi wa helikopta kwa ajili ya kufanya utafiti wa kina wa maeneo yenye madini na kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata taarifa sahihi na kuondokana na uchimbaji wa kubahatisha.

Kuhusu kupanda kwa bei na upungufu wa kemikali ya sayanaidi, Waziri Mavunde amesema tarehe 2 Desemba 2025 kutafanyika kikao maalum kati ya Wizara ya Madini, Tume ya Madini na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali ili kutafuta suluhisho  na hatua za kukabiliana na hali hiyo kwa wachimbaji wadogo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Nyang’hwale, Grace Kingalame, amempongeza Waziri Mavunde kwa usimamizi imara unaoendelea kuinufaisha jamii ya wachimbaji wadogo.

Naye, Mbunge wa Nyang’hwale, Mhe. Hussein Nassor Amar, ameomba leseni za utafiti ambazo hazifanywi kazi zifutwe na kugawiwa kwa wachimbaji wadogo.

Pia, Mwenyekiti wa Vijana Wachimbaji Madini Taifa, Khamis Mohamed, amemshukuru Waziri kwa kuendeleza programu ya MBT, na kuomba maeneo yenye taarifa sahihi ya uwepo wa madini yatengwe kwa ajili ya vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum.

Mwisho, Waziri Mavunde ametoa wito wa kudumisha amani katika maeneo yote ya uchimbaji.

“Tanzania ni nchi ya amani. Naomba tuendelee kuilinda kwa wivu mkubwa na kuheshimiana katika shughuli za uchimbaji,” amewaasa wachimbaji madini nchi.
Posted by MROKI On Saturday, November 29, 2025 No comments

November 27, 2025



Na Wandishi wetu, Simanjiro,Manyara
Serikali imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuimarisha ushiriki wa Watanzania katika uchumi wa madini kupitia programu jumuishi ya Mining for Better Tomorrow (MBT), inayolenga kuwawezesha vijana na wanawake kunufaika moja kwa moja na rasilimali za taifa.

Dhamira hiyo imesisitizwa leo, Novemba 27, 2025, na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde, wakati akizungumza na mamia ya wachimbaji wadogo vijana katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Lemshuku, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara.

Akizungumza kwa msisitizo, Waziri Mavunde amesema anataka kuona uchumi wa madini nchini ukimilikiwa na Watanzania wenyewe, na kwamba Tanzania inakuwa kitovu cha biashara ya madini barani Afrika endapo yatawekewa miundombinu sahihi na uwezeshaji kwa wananchi.

“Natamani kuona Mirerani, Arusha, Geita, Chunya, Mara,Kahama na maeneo mengine nchini yanakuwa kitovu cha biashara ya madini ya vito na metali Afrika. Nataka kuona Dubai ikihamia Simanjiro,” amesema Mavunde huku akishangiliwa na wachimbaji vijana.

Zaidi ya vikundi 21 vyenye jumla ya wanachama 423 vimekabidhiwa leseni katika ziara hiyo, ambayo vikundi 7 vyenye jumla ya wachimbaji 127 vimapewa leseni za uchimbaji mdogo wa tanzanite na vikundi 14 vyenye wanachama 296 vimepewa leseni za kufanya biashara ya tanzanite, hatua iliyorasimisha vikundi hivyo kwenye mnyororo wa thamani wa tanzanite.

Katika ziara hiyo, Waziri Mavunde ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo kipya cha ununuzi wa madini cha Lemshuku, mradi unaotarajiwa kuwa mkombozi kwa wachimbaji wadogo kupitia mfumo rasmi wa masoko. Ujenzi huo umefikia asilimia 88, na Waziri amemwelekeza Afisa Madini Mkazi wa Mirerani kuongeza kasi ya ujenzi ili kituo kikamilike na kuanza kufanya kazi mapema iwezekanavyo.

Katika mkutano huo, Waziri ametumia muda kuzungumza moja kwa moja na wachimbaji pamoja wamiliki wa leseni za madini ya vito, akisikiliza changamoto zinazowakabili ambapo ameahidi kuzifanyia kazi mara moja changamoto za maji, miundombinu, umeme, usalama, vibali na huduma za kijamii kwani Serikali ni moja na huduma hizo ni kichocheo muhimu katika maeneo yote yenye shughuli za uchimbaji.

Akikumbusha ahadi alizotoa katika ziara yake ya awali, Waziri Mavunde amesema ujenzi wa kituo cha afya cha Lemshuku nao unaendelea na ujenzi, na juhudi za kuhakikisha wakazi wa eneo hilo wanapata huduma ya maji safi zinaendelea. Huduma hizo zinatarajiwa kuboresha ustawi wa wachimbaji na jamii inayowazunguka.

Kwa kuhitimisha, Waziri Mavunde amewata vijana na watanzania kwa ujumla kulinda amani ya nchi ili kufanya maendeleo na kutimiza majukumu yao maana hawana Tanzania nyingine.
Posted by MROKI On Thursday, November 27, 2025 No comments







📍 Manyara
Waziri wa Madini, *Mhe. Anthony Mavunde (Mb)*, ametembelea na kushuhudia utekelezaji wa utafiti wa kina wa madini kwa kutumia teknolojia ya ndege nyuki (drone) katika Kata ya Basotu, Wilaya Hanang, mkoani Manyara. Utafiti huo wa jiofizikia unalenga kubainisha maeneo yenye hifadhi ya madini utakaopelekea kuanzishwa kwa mgodi mkubwa wa dhahabu wilayani humo.

Ziara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, *Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan* aliyoyatoa wakati akihutubia Bunge Oktoba 13, 2025 ambapo alitaja utafiti wa madini kama kipaumbele kwa mwaka 2025 - 2030 utakaopelekea kufikia angalau asilimia 50 ya utafiti wa kina wa madini nchini ifikapo mwaka 2030.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Mavunde amesema utafiti huo ni hatua muhimu kwa maendeleo ya wananchi wa Hanang na Mkoa wa Manyara kwa ujumla, kwani matokeo yake yanatarajiwa kuongeza ajira, kuvutia uwekezaji na kuchochea utekelezaji wa miradi ya kijamii kupitia leseni za uchimbaji madini.

“Tunatarajia utafiti huu utaleta matokeo chanya yatakayobadilisha maisha ya wananchi. Serikali itaendelea kusimamia sekta hii ili iwe chachu ya maendeleo kwa wote,” amesema Mavunde.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Hanang, *Mhe. Almish Hazal*, amemshukuru Waziri Mavunde kwa kutembelea eneo la mradi huo na kuendelea kusisitiza umuhimu wa tafiti za madini katika wilaya yake pia, ameiomba Wizara ya Madini kuendeleza kasi hiyo katika maeneo mengine ya Hanang yenye uwezekano wa kuwa na madini.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Cobra Resources Ltd, *Bw. Amos Nzungu*, amempongeza Waziri Mavunde kwa ushirikiano na uzalendo anaouonesha kwa kufuatilia utekelezaji wa miradi ya utafiti wa madini na kuahidi kukabidhi matokeo ya utafiti mara tu yatakapokamilika.

Kwa upande wa Meneja wa Kampuni ya SkyPM Solution inayofanya utafiti huo, *Bw. Paul Madata* amesema matumizi ya teknolojia ya ndege nyuki yamerahisisha na kuongeza ufanisi wa utafiti wa awali, kwani inaweza kupima hadi zaidi ya kilomita tatu chini ya uso wa ardhi kwa muda mfupi.

Awali, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Manyara, *Mhandisi Godfrey Nyanda* ametoa taarifa ya maendeleo ya sekta ya madini mkoani hapo, akibainisha kuwa hadi kufikia robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/26 (Julai–Oktoba), wamekusanya asilimia 35.21 ya lengo la makusanyo ya Shilingi Bilioni 2.2 lililopangwa kwa mwaka mzima.

“Tutaendelea kusimamia kikamilifu maagizo ya Mhe. Rais na ya Waziri wetu Mhe. Mavunde ili kuhakikisha sekta ya madini inaendelea kukua na kuimarika hapa Manyara,” amesema Mha. Nyanda.
Posted by MROKI On Thursday, November 27, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo