Nafasi Ya Matangazo

December 13, 2025





Na Mwandishi Wetu, Moshi
Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Bw.  Kiseo Nzowa ametoa wito kwa Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) kuweka utaratibu bora kwa ajili ya klabu shiriki kwenye michezo hiyo, kutumia wachezaji kutoka klabu nyingine.

Bw. Nzowa aliyekuwa mgeni rasmi kwenye mkutano mkuu wa SHIMIWI leo tarehe 12 Desemba, 2025 unaofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi.

Amesema kuwekwe kwa mfumo bora unaowatambulisha, kurasimisha na kuruhusu watumishi wachache kutoka sehemu moja wenye vigezo vya kushiriki kwenye michezo ya SHIMIWI katika michezo mbalimbali iliyopo.

“Kama mnakumbuka kipindi cha nyuma chama cha mpira TFF kilikuwa na kanuni isiyoruhusu wachezaji wa nje ya nchi kucheza kwenye ligi ya Tanzania, lakini baadaye walikaa na kubadilisha utaratibu na sasa wachezaji wa nje wanaruhusiwa, hivyo na sisi SHIMIWI tukae tuone njia nzuri yenye mfumo bora wa kuruhusu hawa wanaotoka sehemu nyingine kushiriki bila kuonekana wasiostahili kwa jina la mamluki,” amesisitiza Bw. Nzowa.

Lakini, Bw. Nzowa pamoja na kuonesha changamoto hiyo ya mamluki, lakini amesema SHIMIWI inamafanikio makubwa kwa kufuata kalenda yao kwa kufuata matukio kama yalivyopangwa kuanzia Januari hadi Desemba.
Posted by MROKI On Saturday, December 13, 2025 No comments




Na Mwandishi Wetu, Moshi
Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Bw. Kiseo Nzowa ameishukuru serikali chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuruhusu michezo ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala za serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI).

Bw. Nzowa aliyekuwa mgeni rasmi leo tarehe 12 Desemba, 2025 kwenye mkutano mkuu wa SHIMIWI unaoendelea kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro amesema serikali imetoa fursa ya kushiriki kwenye michezo ikitambua faida zake za kuwa na michezo mahala pa kazi.

“Ninaishukuru sana serikali kwa kuruhusu michezo ya SHIMIWI kufanyika kila wakati, na hata nyie mmekuwa mkifuata taratibu na kalenda yenu mliyoiweka kwa matukio yenu, hongereni sana,” amesema Bw. Nzowa. 

Hatahivyo, amewataka washiriki kuhakikisha wanaonesha nidhamu ya juu katika matukio mbalimbali ya shiririkisho hili.

Halikadhali, Bw. Nzowa ametoa angalizo kwa klabu shiriki kuhakikisha wanafanya maandalizi ya kutosha ya kushiriki kwenye michezo hiyo mara wapatapo mwaliko wa kushiriki, ili waweze kufanya vizuri.

“Hili la watumishi kukosa maandalizi mazuri kuna mawili aidha barua ya mwaliko imechelewa kuwafikia au kiongozi mwenye mamlaka kuamua kutowaruhusu kwa madai ya kuwa na kazi nyingi, suala la ushiriki wa michezo lipo kisheria kwa kuwa inawajengea watumishi afya bora na kuwafanya wawe na bidii katika kazi za kuwahudumia wananchi,” amesema Bw. Nzowa.

Awali kwa upande wake Mwenyekiti wa SHIMIWI, Bw. Daniel Mwalusamba amemshukuru Rais Samia kwa kuendelea kuruhusu watumishi wa umma kufanya mazoezi na kushiriki michezo mahali pa kazi kwa kujenga afya zao na kuwawezesha kushiriki vyema kwenye kazi za kujenga taifa.

Bw. Mwalusamba, pia amemshukuru mgeni rasmi kwa kuitikia wito wa kushiriki kwenye mkutano huu ambao upo kikatiba, kwani amewapa faraja viongozi wa michezo na pia kuwapa chachu ya kuendelea kufanya kazi kwa bidii, wanaamini uongozi thabiti wa RAS utaendelea kuwaongoza vyema katika utendaji kazi.

“Nisiwe mchoyo wa fadhila ninawashukuru viongozi wa mahala pa kazi kwa kuendelea kuwaruhusu watumishi wao mahala pa kazi kuja kushiriki matukio mbalimbali ya SHIMIWI, na tunawaomba waendelee kuwa na moyo huo, na pia tunaishukuru ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kwa kufanikisha bega kwa bega mkutano huu, ambao umefanikiwa,” amesema Bw. Mwalusamba.
Posted by MROKI On Saturday, December 13, 2025 No comments

December 12, 2025






Na Mwandishi wetu, Arusha
Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amemtaka mkandarasi wa ujenzi wa kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) kukamilisha ujenzi wa majengo ya kituo cha mafunzo ya  Uongezaji thamani madini ya vito kwa kuongeza nguvukazi na kufanya kazi kwa masaa 24 ili kukamilisha ujenzi wa jengo kwa muda mfupi.

Waziri Mavunde ameyasema hayo leo Desemba 12, 2025 mkoani Arusha  wakati wa ziara yake ya  kukagua mradi wa kituo hicho  ulioanza ujenzi rasmi ambapo katika maelekezo yake amemtaka mkandarasi kuzingatia ujenzi bora wenye kukidhi vigezo vilivyoainishwa kwenye mkataba.

Waziri Mavunde amefafanua kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais.Dkt. Samia Suluhu Hassan  inatekeleza mikakati yake kwenye mnyororo mzima wa uongezaji thamani madini ya vito kama Sera ya Madini ya Mwaka 2009 inavyoelekeza.

Sambamba na hapo, Waziri Mavunde amesisitiza kuwa,  kuanza kwa ujenzi huu ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa Mhe. Rais. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati akihutubia Bunge la 13 jijini Dodoma.

Waziri Mavunde amebainisha kuwa,  kukamilika kwa  kituo hicho , kutaleta faida mbalimbali ikiwa pamoja na kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi watakao jiunga kwenye kituo, kuongezeka kwa wataalamu wa uongezaji thamani madini ya vito, kufungua fursa za ajira kwa vijana na wafanyabiashara wa madini , pamoja na kutosafirishwa kwa madini ghafi nje ya nchi hivyo kutachagiza  ongezeko la  mapato kwa taifa.

Kwa upande wake , Mkuu wa Wilaya Arusha Mhe. Joseph Mkude ameahidi kuendelea kufuatilia maendeleo ya ujenzi ili kuhakikisha ujenzi unakamilika kama Serikali inavyotaka.

Mkude ameongeza kuwa, kukamilka kwa kituo hicho itakuwa moja ya sehemu ya uwekezaji mkubwa wa serikali  husasan kwenye Sekta ya Madini mkoani Arusha.

Awali, akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi, Mkuu wa kituo cha TGC Mhandisi. Ally Maganga ameeleza kuwa, ujenzi wa majengo pacha hayo ya ghorofa 8 utagharimu Tsh Bilioni 33 na kukamilika kwake kutaongeza fursa ya vijana wengi kupata ajira kupitia ujuzi wa uongezaji thamani madini ya vito.

Naye Meneja Mradi Mhandisi Robert Lubuva ameahidi kuhakikisha kama wakandarasi wataongeza nguvu ya rasilimali watu na vifaa ili mradi uweze kukamilika na kuwahudumia watanzania kwa wakati.
Posted by MROKI On Friday, December 12, 2025 No comments




Rombo- Kilimanjaro
Serikali imeeleza kujivunia hatua kubwa zinazopigwa na Wachimbaji Wadogo nchini, wakiwemo wanaochimba Madini ya Pozzolana pamoja na wakataji wa matofali ya volcano (volcanic blocks) katika Kata ya Holili, Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro, hatua inayoendelea kuonesha kasi ya ukuaji wa Sekta ya Madini siku hadi siku.

Kauli hiyo imetolewa leo Desemba 11, 2025 na Naibu Waziri wa Madini, Mhe. Dkt. Steven Kiruswa wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli za uchimbaji wilayani Rombo, ambapo amesisitiza kuwa Sekta ya Madini imekuwa mhimili unaochochea na kuunganisha sekta nyingine kama ujenzi, viwanda, biashara, kilimo, maji na maeneo mengine ya uchumi.

Dkt. Kiruswa amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini imeanzisha Programu ya Mining for A Brighter Tomorrow – MBT yenye lengo la kuwawezesha vijana na wanawake wanaojihusisha na uchimbaji mdogo kwa kuwapatia leseni za uchimbaji pamoja na vifaa vya kisasa ili kuboresha uzalishaji wao na kuongeza tija.

 “Programu hii ni sehemu ya dhamira ya Serikali kuhakikisha wachimbaji wadogo wanapiga hatua na kuwa sehemu pana ya uchumi wa taifa,” amesema Dkt. Kiruswa.

Katika hatua nyingine, Dkt. Kiruswa ameongeza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini itaendelea kufuta leseni za uchimbaji na utafiti ambazo hazifanyiwi kazi, ili kuhakikisha rasilimali madini zinawanufaisha Watanzania kikamilifu na kuondoa vizuizi vinavyochelewesha maendeleo ya sekta.

Kwa upande, Mkuu wa Wilaya ya Rombo,  Mhe. Raymond Mwangwala amesema kuwa uwepo wa madini ya Pozzolana umesaidia kutangaza Wilaya hiyo sambamba na kuongeza mapato ya Halmashauri ya Wilaya ya Rombo huku vijana wakinufaika na ajira kupitia uwepo wa madini hayo yatokanayo na volcano na miamba ya volcano inayotumika kutengenezea matofali imara.

Kwa upande wake Afisa Madini Mkazi wa Mkoa Kilimanjaro Mhandisi Abel Madaha ameeleza kuwa makusanyo ya maduhuli kutoka Sekta ya Madini katika Mkoa wa Kilimanjaro yamefikia shilingi bilioni 1.63 kuanzia Julai hadi Novemba 2025, ikiwa ni asilimia 45 ya lengo la mwaka la kukusanya shilingi bilioni 4.2 kwa mwaka wa fedha 2025/2026, hatua imayoashiria mwitikio mzuri wa wachimbaji na usimamizi madhubuti unaoendelea kufanywa na Wizara ya Madini ili kuhakikisha rasilimali za nchi zinachangia kikamilifu kwenye maendeleo ya taifa.

Pozzolana ni aina ya madini ujenzi yenye asili ya udongo au majivu ya volkano ambayo, ikichanganywa na chokaa na maji, huunda saruji yenye uimara mkubwa na hutumika kwa wingi katika viwanda vya saruji hapa nchini.
Posted by MROKI On Friday, December 12, 2025 No comments



Na Jackline Minja MJJWM-
Dodoma
Serikali ya Awamu ya Sita, inaendelea kuweka kipaumbele katika ajenda ya ustawi na mifumo ya ulinzi wa mtoto, kuendeleza huduma za malezi mbadala, usimamizi wa Makao ya Watoto nchini ili kuhakikisha yanatoa huduma kwa viwango vinavyotakiwa.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi wakati wa ziara ya kutembelea Makao ya Watoto ya Taifa Kikombo Jijini Dodoma na kujionea huduma zinazotolewa katika Makao hayo.

Mhe. Maryprisca amesema Makao ya Taifa ya Kikombo ni mfano wa Taasisi ya Serikali inayotekeleza majukumu hayo kwa weledi, upendo na dhamira ya dhati.

“Nimetembelea miradi, miundombinu na kupokea taarifa ya mafanikio, changamoto na maeneo yanayohitaji kuimarishwa, nafurahishwa kuona jitihada kubwa zinazofanywa katika kutoa huduma ya Elimu, Afya, Lishe, ushauri nasaha pamoja na malezi kwa Watoto napenda kuwahakikishia kuwa Wizara itahakikisha Makao haya yanawezeshwa ipasavyo”. amesema Mhe. Maryprisca.

Aidha Mhe. Maryprisca ametoa rai kwa wadau wa maendeleo, mashirika ya kiraia, sekta binafsi na jamii kuendelea kushirikiana na Wizara kwa kuwapa watoto fursa sawa za maendeleo kama ilivyo kwa watoto wengine wote wa Tanzania.

“Niwaombe Mashirika, wadau wa maendeleo tuendelee kuiunga mkono Serikali katika kuendeleza makazi ya watoto ili wawe na huduma nzuri na wasijione wanyonge na niwaambie kuwa ninyi ni watu muhimu, mnapendwa na Taifa linawahitaji, msipoteze matumaini, someni kwa bidii, zingatieni maadili, muwe na nidhamu na mtumie fursa mnazopata ili mkafikie ndoto zenu."
amesema Mhe Maryprisca

Katika hatua nyingine Mhe. Maryprisca ameupongeza Uongozi wa Makao ya Taifa ya Kikombo kwa kazi wanayoifanya na kuwataka kuendeleza ushirikiano ili kuhakikisha kuwa kila mtoto analelewa katika mazingira salama, yenye upendo na yenye kumjenga.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Wakili Amon Mpanju amesema watumishi wa Makao hayo wana weledi na uwezo mkubwa wa kutambua uwezo wa watoto  licha ya changamoto wanazokuja nazo watoto katika makazi hayo.

“Hawa watumishi unaowona hapa wanauwezo wa kukaa nao, kuongea nao kwa mbinu tofauti ndio maana nasema hawa sio watu wakawaida hata mimi wakiniangalia wanasema hapo hauko sawa, lakini ni miongoni mwa watu walioaminiwa na Serikali ambao watatusaidia kukiendeleza Makao haya”. amesema Wakili Mpanju.

Awali akisoma taarifa ya huduma zinazotolewa katika makao ya Taifa ya watoto kikombo Afisa Ustawi wa Jamii Anord Fyataga amesema hadi sasa kituo kimepata mafanikio mengi ikiwemo kuimarika kwa huduma za ushauri na unasihi ambapo kila mtoto anapata ushauri wa moja kwa moja au wa makundi ,kuunganisha watoto 20 na familia zao, kuboreshwa kwa huduma za elimu ndani na nje ya makao ambapo wastani wa ufaulu wa watoto kwa shule za msingi na sekondari umeongezeka kwa asilimia mbili (2%) pamoja na kuwajengea ujuzi watoto 40 katika ujifunzaji wa stadi mbalimbali za maisha makaoni kama ushonaji wa nguo kwa kutumia cherehani.
Posted by MROKI On Friday, December 12, 2025 No comments

December 11, 2025








Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema kuwa mradi wa upanuzi wa Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Kinyerezi 1 Extension umekamilika rasmi, ikiwa ni pamoja na kufungwa kwa Transfoma yenye uwezo wa MVA 175.

Amesema hatua hii ni muhimu kwa kuboresha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa Jiji la Dar es Salaam, hususan maeneo ya Mbagala na Gongo la Mboto, ambayo yamekuwa yakikumbwa na changamoto za kukatika kwa umeme kutokana na ongezeko la watu na shughuli za kiuchumi.

Mhe. Salome amesema hayo Desemba 11, 2025, wakati wa ziara yake katika vituo vya uzalishaji umeme vya Kinyerezi I, Kinyerezi II, Ubungo I, Ubungo II na Ubungo III akiongeza kuwa mradi tayari umeanza majaribio (testing).

“Tunamshukuru sana Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa. Transfoma zimefungwa, majaribio yanaendelea, na wananchi wa Gongo la Mboto na Mbagala sasa watapata umeme wa uhakika,” Mhe. Salome.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema Shirika linaendelea kuboresha miundombinu yake ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka.

Amebainisha kuwa katika eneo la Kinyerezi kumefungwa Transfoma kubwa ya MVA 175, huku maeneo ya Gongo la Mboto na Mbagala yakiwekewa Transfoma ya MVA 120 ili kukidhi ongezeko la mahitaji ya umeme.

Amesisitiza kuwa idadi ya watu imekuwa ikiongezeka Jiji la  Dar es Salaam, hivyo miundombinu ya umeme lazima iboreshwe mara kwa mara ili kuendana na uhitaji uliopo. 

"Lengo la Kinyerezi 1 Extension lilikuwa kuongeza uwezo wa kusambaza umeme unaozalishwa kuwafikia wateja wetu kwa kiwango kinachostahili," amesema Bw. Twange.
Posted by MROKI On Thursday, December 11, 2025 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ametuma salam za pole na kusikitishwa kwa kifo cha Mhe. Jenista Mhagama aliyekua Mbunge wa Jimbo la Peramiho kilichotokea hii leo.

Katika Salam hizo Rais Samia amesema "Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama. Ninatoa pole kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu, wananchi wa Jimbo la Peramiho, familia, ndugu, jamaa na marafiki. 

Kwa miaka 38, Mheshimiwa Mhagama amekuwa mwanachama mahiri wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kiongozi wa vijana, kiongozi wa wanawake, waziri katika awamu mbalimbali na mnasihi wa wengi katika siasa na maisha. 

Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. 
Amina." 
Posted by MROKI On Thursday, December 11, 2025 No comments




 

Posted by MROKI On Thursday, December 11, 2025 No comments

December 10, 2025


Na Mwandishi Maalumu – Dar es Salaam
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge ameibuka mshindi wa Tuzo ya Mkurugenzi Mtendaji Bora wa Mwaka 2025 iliyotolewa na kampuni ya Eastern Star Consulting Group kwa ushirikiano na CEO Roundtable South Africa.
Tuzo hiyo imetolewa hivi karibuni katika Ukumbi wa SuperDome jijini Dar es Salaam, wakati wa hafla maalumu ya kuwatambua viongozi 100 bora na mahiri barani Afrika wanaotoa mchango mkubwa katika maendeleo ya jamii.
Kwa mujibu wa waandaaji, tuzo hizo hutolewa kwa watendaji wanaodhihirisha ubunifu, uwajibikaji na matokeo chanya katika utendaji wao wa kila siku.
Dkt. Kisenge ametambuliwa kwa uongozi wake thabiti unaoweka mbele maslahi ya wananchi, hususan katika kuboresha huduma za tiba ya moyo nchini—jukumu ambalo limeifanya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)  kuwa kitovu muhimu cha matibabu ya moyo katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Kupatikana kwa Dkt. Kisenge katika orodha ya viongozi 100 bora Afrika ni ishara ya kutambuliwa kimataifa kwa jitihada zake za kusimamia rasilimali, kuboresha miundombinu ya tiba na kuikuza taasisi ya JKCI katika ngazi ya kimataifa.
Chini ya uongozi wake, JKCI imepanua wigo wa huduma za uchunguzi na upasuaji wa moyo, huku idadi ya wagonjwa wanaopatiwa matibabu ndani ya nchi ikiongezeka kwa kasi. Huduma mpya za kitabibu zimeanzishwa, wataalamu wa ndani wamejengewa uwezo kupitia mafunzo ya kisasa na taasisi imeendelea kutekeleza miradi ya utafiti inayolenga kupunguza mzigo wa magonjwa ya moyo nchini.
Baadhi ya wagonjwa wanaohudumiwa na JKCI wamepongeza ushindi huo wakisema ni uthibitisho wa ubora wa huduma na uwajibikaji wa uongozi wa taasisi hiyo.
“Nimekuwa nikitibiwa hapa kwa miezi kadhaa na nimeona jinsi huduma zilivyo bora na za haraka. Kila mfanyakazi anaonekana kujituma na kuwajali wagonjwa. Bila shaka tuzo hii anastahili kabisa kuipata Mkurugenzi wao,” alisema Asha Bakari mmoja wa wagonjwa.
Joseph Mushi anayehudumiwa na taasisi hiyo kwa muda mrefu alisema tuzo hiyo ni fahari sio tu kwa JKCI bali pia kwa wananchi wanaonufaika na huduma zake.
“Zamani tulisikia watu wakisafiri kwenda nje ya nchi kutibiwa, lakini sasa huduma bora zinapatikana hapa hapa nchini. Uongozi wa Dkt. Kisenge umeleta mageuzi makubwa,” alisema.
Hafla hiyo ilihudhuriwa  na washiriki kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania, Kenya, Uganda, Zambia, Malawi na Afrika Kusini ambapo viongozi waliotoa mchango mkubwa katika sekta zao wametambuliwa rasmi.
Posted by MROKI On Wednesday, December 10, 2025 No comments


Na Mwandishi wetu, Rukwa
Kampuni ya Noble Helium kutoka Australia imetangaza mpango wa kuajiri zaidi ya vijana 50 kupitia utafiti mpya wa Helium unaotarajiwa kuanza mwezi Desemba hadi Februari katika kijiji cha Kinambo, Wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa.

Akizungumza kupitia mahojiano maalum hivi karibuni Mwakilishi wa Kampuni hiyo, Pius Simeon Mwita, alisema Noble Helium imefanikisha tafiti mbalimbali za awali na kubaini viashiria muhimu vya uwepo wa gesi ya Helium, huku ikichangia ajira na maendeleo kwa jamii zinazozunguka maeneo ya uchimbaji.

Mwita alisema katika tafiti zilizopita kampuni ilitoa ajira zisizo rasmi zipatazo 450, na pia ilishirikisha wananchi kwenye utoaji wa huduma kama ulinzi, usambazaji wa bidhaa, vilainishi kwa shughuli za uchorongaji, zabuni ndogo, ununuzi wa chakula pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya barabara.

Aidha, alisema Noble Helium imekamilisha tathmini na ulipaji wa fidia kwa wananchi waliopo katika maeneo ya leseni ya utafiti wa Helium, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha shughuli za kampuni zinaendeshwa kwa kuzingatia maslahi ya jamii na sheria za nchi.

Kwa mujibu wa Mwita, utafiti mpya utakaofanyika Kinambo utaongeza nafasi nyingine zaidi 50 kwa vijana, na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika eneo hilo. 

“Tunawaomba vijana wajitokeze kwa wingi pindi fursa hizi zitakapotangazwa. Lengo letu ni kuhakikisha jamii inanufaika moja kwa moja na uwekezaji huu,” alisema.

Utafiti huo unatarajiwa kuongeza kasi ya maandalizi ya uwekezaji mkubwa wa Helium nchini, gesi ambayo imekuwa na mahitaji makubwa duniani kwa matumizi ya teknolojia za tiba, anga na vifaa vya sayansi.
Posted by MROKI On Wednesday, December 10, 2025 No comments
Tungependa tena kuendelea kutoa taarifa ya mwendelezo wa hali ya usalama hapa nchini kuanzia saa 12 asubuhi ya leo ya tarehe 10.12.2025 hadi mchana huu.

Hali ya usalama ni shwari na shughuli za kiuchumi na kijamii zinaendelea kama kawaida nchi nzima baada ya mapumziko ya jana tarehe 9.12.2025 ya sherehe za sikukuu ya Uhuru wa Taifa letu.

Jeshi la Polisi kwa ushirikiano na Vyombo vingine vya ulinzi na usalama vitaendelea kushirikiana na nyinyi wananchi kuhakikisha amani na usalama unaendelea kuimarika hapa nchini ili hata wale wachache wenye hofu waweze kutoka waendelee na shughuli zao za kila siku za kujitafutia riziki na kupata huduma za kijamii wanazo hitaji.

Aidha, tuna washukuru na kuwapongeza wananchi wote kwa nafasi zao kwa namna wanavyoendelea kuwakataa na kuwapuuza wale wanaohamasisha na kuchochea vurugu na ukiukwaji wa Sheria za nchi kupitia mitandao ya kijamii na njia zingine.

Aidha, tuna toa rai kwa kila mmoja wetu tuendelee kuungana kwa pamoja kulinda na kuimarisha amani na usalama wa Taifa letu ili liendelee kuwa sehemu salama ya kuishi kwa vizazi vya sasa na vitakavyo kuja. 


Posted by MROKI On Wednesday, December 10, 2025 No comments
Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, akitoa maelezo ya awali kuhusu mafunnzo ya usalama na afya kazini yalitolewa na OSHA kwa wanawake wanaojihusisha na uzalishaji wa bidhaa za batiki Dar es Salaam 
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo ambaye ameelezea umuhimu wa mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa makundi ya wajasiriamali wadogo huku akiitaka OSHA kuhakikisha mafunzo hayo yanakuwa endelevu. 
Na Fredy Mgunda
Wanawake zaidi ya 200 wanaojihusisha na utengenezaji bidhaa za batiki wamenufaika na mafunzo ya usalama na afya yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kufanya shughuli zao za kila siku kwa kuzingatia kanuni bora za usalama na afya mahali pa kazi.

Mafunzo hayo ya siku moja yaliyogharamiwa na serikali yametolewa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA)  katika eneo la Ilala Jijini Dar es Salaam ambapo mada mbalimbali zikiwemo dhana ya usalama na afya mahali pa kazi, vihatarishi vya usalama na afya katika shughuli za uzalishaji bidhaa za batiki pamoja huduma ya kwanza mahali pa kazi zimefundishwa.

Mafunzo hayo yamefunguliwa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo ambaye ameelezea umuhimu wa mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa makundi ya wajasiriamali wadogo huku akiitaka OSHA kuhakikisha mafunzo hayo yanakuwa endelevu. 

“Wajasiriamali wadogo ni kundi muhimu sana na lenye mchango mkubwa katika kukuza  uchumi wa Taifa letu hivyo ni muhimu kuwapatia mafunzo ili waweze kutekeleza shughuli zao katika hali ya usalama,” amesema Naibu Waziri.

Aidha, amesisitiza kuwa mafunzo hayo yatasaidia kupunguza ajali, magonjwa na vifo vinavyoweza kutokea kutokana ukosefu wa mifumo ya usalama na afya ikiwemo wafanyakazi wenye uelewa wa masuala husika. 

Sambamba na hayo, ametoa wito kwa wafanyabiashara hao kutojihusisha na makundi yenye nia ya kuvuruga shughuli za uzalishaji na kuvunja amani ya nchi ya Tanzania. 

Awali, Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, amesema mafunzo hayo ni mwendelezo wa utekelezaji wa program atamizi ya wajasiriamali wadogo ya Taasisi hiyo ijulikanayo- Afya Yangu, Mtaji Wangu.

“OSHA ilibuni na kutekeleza program ya Afya Yangu-Mtaji Wangu ili kuziba mwanya wa uelewa wa masuala ya usalama na afya uliopo baina ya sekta rasmi na sekta isiyo rasmi hivyo kupitia program hii tumekuwa tukiainisha makundi mbalimbali ya wajasiriamali wadogo na kuyawezesha kwa mafunzo pamoja na kuwapatia vifaa kinga muhimu kutegemeana na aina ya shughuli zao,” amesema Mtendaji Mkuu wa OSHA.

Aidha, amesema program hiyo itaendelea kutolewa kwa makundi mbalimbali hususan vijana ambao kwa mujibu wa tafiti za OSHA za hivi karibuni ndio waathirika wakubwa wa ajali katika maeneo ya uzalishaji kutokana na uelewa mdogo na ukosefu wa uzoefu kazini. 

Akitoa maoni yake katika mafunzo hayo, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Jesca Charles, ameishukuru OSHA kwa kuwapatia elimu na vifaa kinga ambavyo vitawasaidia kujikinga dhidi ya vihatarishi vya ajali na magonjwa hususan kemikali ambacho ndio kihatarishi kikubwa katika uzalishaji wa bidhaa za batiki. 
Posted by MROKI On Wednesday, December 10, 2025 No comments

December 09, 2025


 Na Mwandishi Wetu
Mashabiki wa michezo na wakimbiaji nchini wanatarajiwa kujitokeza kwa wingi kwenye The SQF Zanzibar Cleft Marathon – Season 7, mbio maalum zinazolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto waliozaliwa na tatizo la mdomo na taya wazi (cleft).

Mbio hizo zimepangwa kufanyika Desemba 21, 2025 katika viwanja vya New Aman Complex visiwani Zanzibar, na zimekuwa kivutio kikubwa kwa wanamichezo, wadau wa afya, pamoja na wananchi wanaoguswa na masuala ya kijamii.

Kwa mujibu wa waandaaji, The Same Qualities Foundation (SQF), usajili kwa ajili ya mbio za mwaka huu umeshaanza katika maeneo mbalimbali ikiwemo New Aman Complex, Michenzani Mall, Forodhani, Masomo Bookshop, pamoja na Hospitali ya Edward Michaud jijini Dar es Salaam. Ada ya usajili ni shilingi 35,000 kwa washiriki wa mbio za 21KM, 10KM na 5KM.

Tukio hili ni zaidi ya mashindano, wamesema waandaaji. “Kila hatua unayokimbia ni sehemu ya kubadilisha maisha ya mtoto mmoja—kutoa tabasamu jipya, kuondoa unyanyapaa, na kurejesha matumaini kwa familia nzima.”

Mbio hizi zimepata pia heshima ya kuhudhuriwa na Mgeni Rasmi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, hatua inayoongeza uzito na hamasa kwa washiriki.

Kwa upande wao, wadau wa michezo wamepongeza juhudi za SQF kwa kuunganisha michezo na huduma za kijamii, wakisema mbio hizi zimekuwa mfano bora wa jinsi nguvu ya umoja inaweza kubadili maisha ya watu wanaohitaji msaada.

Waandaaji wametoa wito kwa wakimbiaji, klabu za michezo, mashirika na familia kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuchangia. Washiriki wanaweza pia kulipia kupitia M-Pesa kwa namba 5427230 (The Same Qualities Foundation).

Mbio hizi zinatarajiwa kuwa miongoni mwa matukio makubwa ya michezo ya kijamii mwaka 2025 nchini, yakileta pamoja wanamichezo, wafadhili na watu wa kada mbalimbali kwa lengo moja—kupigania tabasamu la mtoto.
Posted by MROKI On Tuesday, December 09, 2025 No comments

December 08, 2025








Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amefanya ziara katika  Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kwa lengo la kuzungumza na Watendaji taasisi hizo mara baada ya kuteuliwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kushika nyadhifa hiyo  ambapo amewataka watendaji kuhakikisha  Watanzania wananufaika moja kwa moja na uwepo wa rasilimali za mafuta na gesi.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam, Mhe. Salome ameweka mkazo kuhusu upatikanaji wa ajira kwa Watanzania, huduma za kijamii na upatikanaji wa nishati kwa gharama nafuu. 

Mhe. Salome pia ameielekeza Menejimenti ya TPDC kuongeza kasi ya usambazaji wa gesi asilia majumbani ili Watanzania waendelee kunufaika zaidi na rasilimali hiyo muhimu.

Vilevile  ameipongeza TPDC kwa jitihada wanazoendelea kufanya katika utafutaji na uendelezaji wa rasilimali za mafuta na gesi asilia nchini kwani uboreshaji huo umeanza kuleta matokeo chanya katika upatikanaji wa nishati hiyo katika maeneo mbalimbali nchini huku akiwataka kuhakikisha jitihada hizo zinawanufaisha wananchi wengi zaidi.

Katika hatua nyingine, Mhe. Salome amewapongeza PURA kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kuhakikisha sekta ya mafuta inakua nchini huku akiwahimiza kuhakikisha mazingira ya uwekezaji yanakuwa rafiki kwa wawekezaji wapya ili kuongeza ajira na kuhakikisha wananchi wanapata manufaa ya moja kwa moja kutokana na rasilimali na uwekezaji uliopo nchini.  

Aidha, amesisitiza kuwa miradi ya utafiti na uendelezaji wa gesi asilia, ikiwemo mradi wa LNG, ipewe kipaumbele ili kuongeza tija katika uwekezaji na kuhakikisha nchi inanufaika kikamilifu na rasilimali zake huku akisisitiza kuwa taasisi zote zilizo chini ya Wizara lazima ziweke mbele maslahi ya wananchi wakati wa kusimamia miradi ya kimkakati ya nishati lakini pia kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali kuhusu usimamizi, matumizi na faida za rasilimali za gesi asilia.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio amewasisitiza TPDC kuongeza kasi ya uzalishaji na upatikanaji wa  gesi ili nishati hiyo iwe ya kutosha na inawafikia wananchi huku akiisisitiza PURA kuhakikisha wanawapa wawekezaji kipaumbele katika kuwekeza katika fursa za mafuta na gesi kwa lengo la kuhakikisha Serikali inapata mapato na wananchi wananufaika na miradi hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC Mussa Makame amesema shirika linaendelea kuimarisha miundombinu ya kuhifadhi na kusafirisha nishati ya mafuta na gesi, huku likiandaa vizuri upande wa maboresho ya masoko ili kuongeza ufanisi na upatikanaji wa bidhaa hizo nchini na kueleza kuwa kampuni ipo kwenye hatua za kufanya upanuzi wa miradi ya gesi, ikiwemo utekelezaji wa miradi midogo ya LNG itakayowezesha kusafirisha gesi hiyo katika mikoa mbalimbali kwa gharama nafuu na kwa wakati.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Eng. Charles Sangweni amesema PURA itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi huku ikichangia kufanikisha malengo ya sekta kwa mujibu wa Dira ya Taifa 2050.
Posted by MROKI On Monday, December 08, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo