Nafasi Ya Matangazo

January 28, 2026

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Serikali kupitia Wizara ya Madini inaendelea na mchakato wa kuanzisha Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Jiosayansi Tanzania (Tanzania Geoscientists Registration Board – TGRB), ambapo kwa sasa ipo katika hatua ya kukusanya maoni na mapendekezo ya wadau kabla ya kuanzishwa rasmi kwa bodi hiyo.

Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, amesema hayo leo Januari 28, 2026, Bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Bukene, Mhe. Stephano Luhende, aliyetaka kufahamu ni lini Serikali itakamilisha mchakato wa kuanzisha bodi hiyo ili kuongeza ufanisi katika sekta ya madini nchini.

Dkt. Kiruswa ameeleza kuwa baadhi ya taratibu tayari zimekwisha tekelezwa, ikiwemo uandaaji wa rasimu ya Waraka wa Mapendekezo ya Baraza la Mawaziri kuhusu kuanzishwa kwa Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Jiosayansi Tanzania.

Amefafanua kuwa kwa sasa Wizara ya Madini inaendelea na zoezi la kukusanya na kuchambua maoni na mapendekezo kutoka kwa wadau mbalimbali kuhusu masuala yatakayowezesha bodi hiyo kuanzishwa na kujiendesha kwa ufanisi, ikiwemo masuala ya uendeshaji na vyanzo vya fedha.

Ameongeza kuwa mara baada ya kukamilika kwa zoezi la ukusanyaji na uchambuzi wa maoni, Wizara itawasilisha waraka huo katika ngazi za maamuzi za Serikali, ambazo ni kikao cha kitaalamu cha Makatibu Wakuu na kikao cha Baraza la Mawaziri, kwa ajili ya kujadiliwa na kupata ridhaa ya kuanzishwa rasmi kwa Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Jiosayansi Tanzania.
Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments






Na Wizara ya Madini Dodoma
Katibu Mkuu Wizara ya Madini Eng. Yahya Samamba ameongoza kikao cha Menejimenti ya Wizara na Taasisi zake kupitia na kujadili hatua za utekelezaji wa Ahadi zilizotolewa Bungeni na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati akiwasilisha Hotuba yake kwa Mwaka wa Fedha 2025/26.

Katika Mwaka wa Fedha 2025/26, Wizara ya Madini pamoja na kuweka mikakati ya kutekelezwa, ilipanga kutekeleza vipaumbele mbalimbali ikiwemo kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali; kuongeza mchango wa Sekta kwenye Pato la Taifa; kuhamasisha uwekezaji na uongezaji thamani madini; kuimarisha uendelezaji minada na maonesho ya madini ya vito, kuongeza uwekezaji kwenye tafiti zake za kina; kuwarasimisha wachimbaji wadogo na kuzijengea uwezo taasisi zake.

Akizungumza katika kikao hicho, Eng. Samamba amesisitiza kutekelezwa kikamilifu kwa ahadi zilizotolewa na Wizara ili kuendelea kuongeza tija kwa taifa kupitia rasilimali madini.

Naye, Katibu Mtendaji Tume ya Madini Eng. Ramadhan Lwamo amesema tayari mzabuni atakayesimamia minada ya kimataifa ya Madini ya vito amekwishapatikana. Kufanyika kwa minada ya kimataifa ya Madini ya vito  pamoja na mambo mengine kutaongeza mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa kupitia fedha za kigeni, kuitangaza Tanzania  na madini yake yanayopatikana nchini, kuvutia uwekezaji zaidi, kuimarisha hadhi ya Tanzania kimataifa kupitia minada hiyo ya madini ya vito, kuwepo kwa bei halisi ya soko, uwazi na kuongeza washiriki wa ndani na kimataifa. Manufaa mengine ni pamoja na kukuza  wachimbaji wa ndani,  masoko ya uhakika ya madini ya vito na bei za uhakika.  

Pamoja na masuala mbalimbali yaliyojadiliwa, taarifa ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) imeeleza kuhusu hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa kiwanda cha kusafisha chumvi katika Mkoa wa Lindi ambapo imeeleza kwamba matarajio ni kuwa ifikapo mwezi Februari, 2026 kiwanda hicho kitaanza kazi na hivyo kuondoa changamoto ya soko kwa wazalishaji wa chumvi.
Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments





Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limefanya ukaguzi wa kitaalamu wa mita za umeme kwa baadhi ya wateja waliowasilisha malalamiko hayo kwa njia za mitandao katika maeneo ya Tabata Kimanga na Kimara Suka jijini Dar es Salaam.

Malalamiko hayo yaliibuliwa na baadhi ya wananchi mitandaoni na kwenye vyombo vya habari kuhusu madai ya umeme kuisha haraka bila sababu ya msingi.

Zoezi hilo lilifanyika Januari 27, 2026, likiongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO, Bi. Irene Gowelle, akiambatana na timu ya wataalamu wa Shirika, kwa lengo la kubaini chanzo halisi cha changamoto hiyo na kujiridhisha kuhusu ufanisi wa utendaji wa mita za wateja.

MATOKEO YA UKAGUZI
Baada ya kufanyiwa vipimo vya kitaalamu, TANESCO imebaini kuwa mita zote zilizokaguliwa zilikuwa salama na zinafanya kazi kwa usahihi, kinyume na madai yaliyokuwa yakitolewa kuwa mita hizo zina kasoro ya kiutendaji.

Hata hivyo, ukaguzi umeonesha kuwa vyanzo vilivyopelekea wateja waliokaguliwa kulalamika umeme kuisha kwa haraka  ni uchakavu wa mtandao wa nyaya za umeme (wiring) ndani ya nyumba, hali iliyosababisha umeme kuvuja bila mtumiaji kugundua. 

Aidha, matumizi holela ya umeme yameonekana kuchangia kwa kiasi kikubwa changamoto hiyo.

Akizungumza kuhusu zoezi hilo, Bi. Gowelle amesema
“Baada ya kuona malalamiko yanaongezeka, tuliona ni muhimu kufika moja kwa moja kwa baadhi ya wateja waliolalamika. Tulifanya ukaguzi wa kitaalamu, tukazima vifaa vya umeme na kufuatilia usomaji wa mita, lakini bado uniti ziliendelea kupungua. Hii ilithibitisha kuwepo kwa hitilafu katika mfumo wa wiring za ndani ya nyumba na sio mita."

Katika nyumba moja iliyopo Tabata, ukaguzi ulibaini kuwa uchakavu wa mtandao wa nyaya (wiring) ulisababisha upotevu wa takribani uniti mbili za umeme, hali iliyomfanya mteja kutumia zaidi ya shilingi 30,000 za ziada kwa mwezi kuliko matumizi yake halisi.

Kwa upande mwingine, katika nyumba ya mteja mmoja eneo la Kimara Suka, timu ya ukaguzi ilishuhudia matumizi yasiyo bora ya umeme, ikiwemo kuwasha taa wakati wa mchana, hali iliyotajwa kuweza kuchangia kuisha kwa umeme kwa.

WATEJA WALIOKAGULIWA
Miongoni mwa wateja waliokaguliwa ni Devotha Kihwelo, mwandishi wa Gazeti la Mwananchi na mkazi wa Tabata, ambaye taarifa yake iliifanya TANESCO kuwajibika kwa kuchukua hatua ya kufanya ukaguzi huo ambapo Baada ya uchunguzi, ilibainika kuwa nyumba aliyokuwa akiishi ilikuwa na hitilafu kwenye wiring ambayo ilikua ya muda mrefu hali iliyosababisha umeme kupotea.

Wateja wengine waliokaguliwa ni John Vincent wa Tabata Kimanga na Crispin Mizambwa wa Kimara Suka. 

Kwao, ukaguzi umebaini kuwa mita zao zilikuwa hazina changamoto yoyote, na matumizi yao ya wastani wa uniti 2–3 kwa siku yaliendana na vifaa walivyokuwa wakitumia.

Kutokana na matokeo hayo, TANESCO ilijiridhisha kuwa madai ya kuisha kwa umeme bila sababu ya msingi hayakusababishwa na ubovu wa mita na kwamba mita zilikua salama na sawa kiutendaji.

USHAURI KWA WATEJA

TANESCO imetoa elimu ya sababu zinazoweza kuchangia umeme kuisha haraka kuwa ni pamoja na ;
Uchakavu wa mtandao wa nyaya za ndani ya nyumba (wiring)
Matumizi holela ya umeme
Matumizi ya vifaa vya zamani ,vilivyokaa muda mrefu au visivyo na ufanisi wa matumizi ya umeme kidogo
Kutotumia vifaa vyenye teknolojia ya matumizi fanisi (energy efficiency)

Bi. Gowelle amewashauri wateja kufanya jaribio rahisi la kujitathmini kabla ya kulalamika “Wateja wazime vifaa vyote vya umeme, wasome kiwango cha uniti, wakae kwa muda usiopungua saa nne, kisha wasome tena. Endapo uniti zitakuwa zimepungua, wawasiliane na TANESCO kwa ukaguzi. Ikiwa hazijapungua, basi changamoto sio mita bali ni matumizi ya vifaa vyao au mfumo wa wiring zao za ndani umechoka.”

WITO KWA UMMA
TANESCO imetoa wito kwa wateja wote wanaokumbana na changamoto za umeme kuisha haraka kuwasiliana na Shirika moja kwa moja kwa msaada badala ya kuamini au kusambaza taarifa zisizothibitishwa , ili kufanyiwa ukaguzi na kupata ufumbuzi wa kitaalamu unaolenga kupunguza gharama zisizo za lazima kwa wateja wake.
Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments






Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya amesema atahakikisha anasimamia kila mwananchi mwenye  uhalali wa kupata hati milki ya eneo lake analomiliki anapata hati.

Akizungumza na wananchi waliojitokeza kwenye Kliniki Maalum ya Ardhi inayoendelea katika Ofisi za Ardhi Mkoa wa Dodoma leo tarehe 28 Januari, 2026 Mhe. Mmuya amesema, upo umuhimu wa kuhakikisha wananchi waliokamilisha taratibu za kumilikishwa wanapata hati zao kwa kuwa wapo waliofuatilia kwa muda mrefu. 

"Nitasimamia kuhakikisha kila mwananchi mwenye uhalali wa kumiliki Ardhi anapata hati yake kwa wakati”  amesema Naibu Waziri Mmuya.

Ili kutoa huduma bora, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi amewataka wataalamu wa Sekta ya Ardhi nchini kuhakikisha wanatoa elimu ya matumizi bora ya ardhi pamoja na jinsi ya kupata hatimiliki za ardhi, hatua aliyoieleza itasaidia kuepusha ujenzi holela  unaoenda kinyume na matumizi yaliyopangwa.

Mhe. Mmuya amesema, Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kusimamia haki ya umiliki wa ardhi kwa vitendo na kuhakikisha wamiliki wa ardhi wanapata hati zao.

Ameeleza kuwa, Serikali inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inawahakikishia wananchi kuendelea kupata huduma za hati katika maeneo mbalimbali nchini.

Ameongeza kuwa, wizara hiyo chini ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo imeweka mkakati wa siku 14 kuhakikisha  kila mwananchi wa Jiji la Dodoma aliyekidhi vigezo vya kupata hati milki ya ardhi anapata hati yake hatua aliyoieleza kuwa,  itaidia kurahisisha huduma na kulinda haki za wananchi.

Awali, Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga amesema, wamiliki wa ardhi waliokamilisha taratibu za umiliki wapewe Hatimiliki zao na hawahitaji maneno mengi.

Mhandisi Sanga amesisitiza kuwa, ni marufuku kwa mtumishi wa sekta ya ardhi anayefutwa na mwanachi mwenye shida kumwambia aende kwa mtu mwingine kupata huduma na kueleza kuwa, atasimamia msimamo huo kwa kuwa mwananchi anachohitaji ni huduma.

Katika siku ya kwanza ya zoezi hilo, tayari zaidi ya Hatimiliki 150 zimetolewa  ambapo Edward Aloyce na Colletha Magema miongoni mwa wananchi waliopata hati zao wamethibitisha kwamba, zoezi hilo ni muhimu na linawasaidia wananchi kupata hati za ardhi kwa lengo la kumiliki maeneo yao kihalali.

Zoezi la Kliniki Maalum ya Ardhi ambayo imejikita kutoa Hatimiliki za Ardhi katika jiji la Dodoma ni la siku 14 kuanzia 28 Januari hadi Februari 10, 2026.
Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akisalimiana na Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye ofisini kwa Waziri Mkuu Mlimwa jijini Dodoma, Januari 28, 2026. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza  na Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye ofisini kwa Waziri Mkuu Mlimwa jijini Dodoma, Januari 28, 2026. 

Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments

Na Jackline Minja MJJWM-Dodoma 
Serikali imesema haina haja ya kuweka sharti la kisheria linalowalazimisha watoto kuwahudumia wazazi wao wasiojiweza, ikieleza kuwa suala hilo tayari linashughulikiwa kupitia misingi ya kifamilia na kijamii.

Kauli hiyo imetolewa bungeni na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa kinondoni Mhe. Tarimba Gulam Abbas lililohoji "Je Serikali haioni haja ya kuweka sharti la kisheria la watoto wakubwa kutunza wazazi wao wasiojiweza"?

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Mahundi amesema Serikali inatambua umuhimu wa familia na jamii katika kuchukua jukumu la kulea na kuwahudumia wazee, akisisitiza kuwa huo ni msingi wa mila na desturi za Watanzania.

Aliongeza kuwa Serikali imeendelea kuimarisha huduma na matunzo kwa wazee kupitia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003, Toleo la mwaka 2024, ambayo inasisitiza wajibu wa familia na jamii katika kuwahudumia wazee wao.

“Serikali inatambua umuhimu mkubwa wa familia na jamii katika kuchukua jukumu la kulea na kutunza wazee, kwani huu ndio msingi wa mila na desturi za Kitanzania na nguzo muhimu katika kujenga mshikamano wa kijamii. Katika kuimarisha huduma na matunzo kwa wazee, Serikali imefanikiwa kufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003 na kuandaa toleo la mwaka 2024, ambalo linaeleza bayana wajibu wa familia na jamii katika kusimamia matunzo ya wazazi na wazee kwa ujumla, Sera hiyo pia imeweka msisitizo wa kuimarisha mifumo ya kisheria utakaolinda na kuendeleza ustawi wa wazee pamoja na watoto wanaowatunza. Kwa sasa Serikali ipo katika hatua ya kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kutoa maoni juu ya masuala muhimu ya kuzingatiwa katika sheria hiyo.”amesema Mhe. Mahundi

Hata hivyo, amebainisha kuwa Serikali itaendelea kuhamasisha maadili ya uwajibikaji wa kifamilia na kuimarisha mifumo ya kijamii inayosaidia ustawi wa wazee nchini.
Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments




Halmashauri ya Mji Ifakara Januari 27,2026 imetoa mikopo ya asilimia 10 yenye thamani ya Shilingi milioni 600 ikiwa ni Mikopo ya Asilimia 10 inayotokana na Mapato ya ndani  kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, ikiwa ni utekelezaji wa sera ya kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Akizungumza wakati wa hafla ya utoaji wa mikopo hiyo iliyofanyika katika Viwanja vya Stendi ya mabasi kibaoni  Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Felista Mdemu, ameipongeza Halmashauri hiyo kwa kuendelea kutekeleza kwa vitendo azma ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia mikopo isiyo na riba.

Mdemu amevitaka vikundi vilivyonufaika kutumia mikopo hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa, kuzingatia masharti ya mikataba, pamoja na kurejesha mikopo kwa wakati ili kutoa fursa kwa wananchi wengine kunufaika.

 Shilingi 404,787,300 tayari imekwishatolewa kwa vikundi 41, vikiwemo vikundi 20 vya wanawake, 17 vya vijana na 4 vya watu wenye ulemavu na  Shilingi 195,212,700 zitatolewa kwa vikundi 17 vilivyosalia mara baada ya kukamilisha maboresho yaliyoelekezwa.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Ifakara, Pilly Kitwana amewasihi wananchi wa Halmashauri ya Mji Ifakara kuendelea kuunda Vikundi kwani pesa bado zipo ambazo zitasaidia kuwainua pia ameahidi kuendelea kufanya tathimini na  ufuatiliaji kwa vikundi vilivyonufaika ili kuhakikisha mikopo hiyo inaleta tija na kuchangia maendeleo ya kiuchumi kwa wanufaika na jamii kwa ujumla.
Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments
Mtaalamu wa tiba viungo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Jackline Mariki akitoa elimu kuhusu afya bora mahala pa kazi wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya kwa wafanyakazi wa Boharai Kuu ya Dawa (MSD) iliyoanza leo katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Aloyce akimuonesha namna uwiano wa uzito na urefu unavyatakiwa kuwa Mfanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) Christopher Komba wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya inayofanywa na wataalamu kutoka JKCI katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya iliyoanza leo katika ofisi za Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Picha na Khamis Mussa
Baadhi ya Wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya iliyoanza leo katika ofisi za Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Picha na Khamis Mussa
****************
Na Mwandishi Maalumu - Dar es Salaam.
27/01/2026 Wafanyakazi wanaotumia muda mwingi maofisini wametakiwa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo shinikizo la juu la damu na magonjwa ya moyo.

Hayo yamesemwa leo jijini Dar es Salaam na Daktari bingwa wa watoto kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theophilly Mushi wakati akitoa mafunzo maalumu kuhusu namna ya kuzuia magonjwa ya moyo na shinikizo la juu la damu katika kambi maalumu ya siku mbili ya upimaji wa afya kwa wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD).  

Akizungumzia hali ya afya nchini, Dkt. Theophilly alisema takwimu za Wizara ya Afya zinaonesha kuwa asilimia 20 ya vijana nchini wanakabiliwa na ugonjwa wa shinikizo la juu la damu, huku upande wa watu wazima tatizo hilo likichukua asilimia 35%.

“Mazingira ya kazi za mijini, kushindwa kupata nafasi ya kufika katika vituo vya afya ili kufanya uchunguzi wa afya, kazi za kukaa muda mrefu ofisini bila mazoezi, vimechangia kwa kiasi kikubwa ongezeko la magonjwa ya moyo miongoni mwa wafanyakazi wanaotumia muda mwingi ofisini”, alisema Dkt. Theophilly

“Magonjwa ya moyo na shikinizo la juu la damu yameendelea kuwa tishio kubwa kwa jamii hususani wafanyakazi wa mijini ndio maana leo tumefika MSD ili kutoa elimu ya afya bora mahali pa kazi, kufanya upimaji wa afya, kuwapa elumu kuhusu umuhimu wa kufanya mazoezi, kuzingatia uzito wenu wa mwili na kuzingatia lishe bora,” alisema Dkt. Theophilly.

Kwa upande wake Mtaalamu wa tiba viungo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Jackline Mariki alisema ni muhimu wafanyakazi wakazingatia afya mahali pa kazi ili kuepuka maumivu ya shingo mabega na mgongo yanayotokana na kukaa kwa muda mrefu na kutokukaa kama inavyotakiwa.

 “Tumeona ni muhimu tukawaelimisha wafanyakazi kuhusu afya mahali pa kazi ili waweze kufahamu namna sahihi ya kukaa, aina ya viti vitakavyowaepusha kupata shida za mgongo, namna nzuri ya kunyanyua vitu na kupanga vifaa ili waweze kujikinga na magonjwa ya viungo vya mwili,” alisema Jackline.

Nao wafanyakazi wa MSD walisema mafunzo waliyoyapata yamewapa uelewa mpana kuhusu umuhimu wa kujali afya zao hivyo kuepuka kupata maradhi yanayoweza kuzuilika endapo hatua za kinga zitazingatiwa ipasavyo.

 “Nawashukuru sana wataalamu wa JKCI kwa kutufiika na kutupa elimu ambayo itanisaidia kujikinga na magonjwa ya moyo, kinga ni bora kuliko tiba nitatumia elimu niliyoipata kufanya mazoezi yatakayoniepusha na magonjwa hayo,” alisema Emanuel Kiunga, Afisa Tehama Mwandamizi kutoka Bohari Kuu ya Dawa (MSD).

 “Kama mfanyakazi ninayetumia muda mwingi kukaa ofisini nimejifunza kupangilia muda wangu ili niweze kupata na muda wa kuchunguza afya yangu na kujilinda na magonjwa yasiyoambukiza, pia nitazingatia ushauri tuliopewa na wataalamu ili afya yangu iwe imara wakati wote,” alisema Dorothy Mtatifikolo.
Posted by MROKI On Wednesday, January 28, 2026 No comments

January 27, 2026



Na Wizara ya Madini, Dodoma
Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, amesema Wizara ya Madini imeandaa rasimu ya Mkataba kati ya Wamiliki wa Leseni za Uchimbaji na Wachimbaji Wadogo, ambao umewasilishwa kwa Maafisa Madini Wakazi nchini kote kwa ajili ya usimamizi pindi utakapokuwa umesainiwa na kusajiliwa.

Dkt. Kiruswa ameyasema hayo leo Januari 27, 2026, Bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu
swali la Mbunge wa Katoro, Mhandisi Kija Ntemi, aliyetaka kufahamu ni nani atasimamia
mikataba kati ya wamiliki wa leseni na wachimbaji wadogo wanaovumbua madini, pamoja
na muda wa mikataba hiyo.

Amesema mikataba hiyo itadumu kwa kipindi cha miaka mitatu na itaweza kuhuishwa kwa kipindi kingine kulingana na makubaliano ya wahusika. ‘’ Mikataba hiyo itadumu kwa kipindi cha miaka mitatu na huruhusiwa kuhuishwa kwa kipindi kingine kulingana na makubaliano ya wahusika,’’amesema Dkt. Kiruswa.

Amefafanua kuwa, kufuatia marekebisho ya Kanuni za Haki za Madini za Mwaka 2018 yaliyofanyika mwaka 2025, Kanuni ya 5A (1) imeweka sharti la mmiliki wa leseni ndogo ya uchimbaji kuingia mkataba na mchimbaji mdogo atakayefanya shughuli za uchimbaji ndani ya eneo la leseni yake, na kuhakikisha mkataba huo unaidhinishwa na kusajiliwa na Tume ya
Madini.

Katika hatua nyingine, akijibu swali la Mbunge wa Tarime Vijijini, Mhe. Mwita Waitara,
aliyetaka kujua ni lini Kanuni za Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) kwenye migodi zitabadilishwa
ili miradi ya maendeleo   isimamiwe na Halmashauri kwa mtindo wa Local Fund badala ya mwekezaji, Dkt. Kiruswa amesema Kanuni ya 15(1) imeelekeza mmiliki wa leseni kuwajibika kutekeleza mpango wa wajibu wake kwa jamii.

Ameeleza kuwa katika utekelezaji wa miradi ya CSR, mmiliki wa leseni anatakiwa
kuzingatia taratibu za ununuzi na anaweza kuajiri mkandarasi au mtu mwingine yeyote kwa ajili ya utekelezaji wa miradi iliyopo kwenye mpango wa CSR.

Aidha amesisitiza kwamba, Kanuni za Wajibu wa Wamiliki wa Leseni kwa Jamii (CSR),
zilizoanza kutumika rasmi mwezi Juni 2023, zinaeleza wazi majukumu ya wadau mbalimbali katika kuhakikisha jamii zinazozunguka migodi zinanufaika ipasavyo na uwepo wa migodi hiyo.

 Ameongeza kuwa utekelezaji wa majukumu hayo unapaswa kufanywa na mmiliki wa
leseni kwa kushirikiana kwa karibu na Mamlaka za Serikali za Mitaa (Halmashauri).
Posted by MROKI On Tuesday, January 27, 2026 No comments

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akiwasilisha hoja ya kujadili hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bungeni jijini Dodoma, Januari
  27, 2026. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kufanya mageuzi ya sera zinazogusa moja kwa moja maslahi na ustawi wa maisha ya wananchi. 

 

Amesisitiza kuwa Serikali haitavumilia watendaji wa Serikali wanaotoa visingizio, wasiowajibika na wenye hulka ya kufanya kazi kwa mazoea, ujanja ujanja na kutoa taarifa za michakato badala ya majibu yanayotakiwa.

 

Amesema hayo Bungeni leo (Jumanne, Januari 27, 2026) wakati akitoa hoja ya kujadili hotuba ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa jijini Dodoma wakati akizindua Bunge la 13 Novemba 14, 2025.

 

“Tunapozungumzia utendaji Serikalini, msisitizo ni uadilifu na uwajibikaji wa Serikali kwa wananchi waliotuchagua ili kuhakikisha wananchi wananufaika na rasilimali za nchi pamoja na kupata huduma wanazostahili.”

 

Dkt. Mwigulu amesema kuwa hotuba aliyoitoa Rais Dkt. Samia ilitoa mwelekeo na dira ya Serikali ya Awamu ya Sita kwa kipindi cha pili. “Hotuba ya Mheshimiwa Rais ilitoa maelekezo na kubainisha changamoto pamoja na majukumu yanayotupasa kuyatekeleza kwa kushirikiana na wananchi na wadau wengine wa maendeleo.”

 

Kadhalika, Waziri Mkuu amesema kuwa Serikali imejipanga kikamilifu kutekeleza vipaumbele vyote vilivyoainishwa. “Serikali imeainisha maeneo mbalimbali ya utekelezaji na kupanga mipango kazi ya utekelezaji wa muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu, na tayari utekelezaji wake umeshaanza kutekelezwa kwenye maeneo kadhaa”.
Posted by MROKI On Tuesday, January 27, 2026 No comments
Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imesema itaendelea kulinda vyanzo vya maji na mito mbalimbali nchini kwa kuzingatia Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 na Sheria ya Rasilimali za Maji ya Mwaka 2009.

Pia, imesisitiza kuwa itashirikiana na Wizara ya Madini kuendelea kutoa elimu kwa wachimbaji na wananchi kwa ujumla kuzingatia sheria na taratibu ili kuwa na mazingira endelevu.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange bungeni jijini Dodoma leo Januari 27, 2026 wakati akijibu swali la Mbunge wa Morogoro Kusini Mhe. Zuberi Mfaume aliyetaka kujua ni hatua gani zimechukuliwa za uchafuzi wa Mto Mfizigo na Mhuva zitokanazo na shughuli za madini na kubaini kemikali zilizopo na athari zake.

Akiendelea kujibu swali hilo Mhe. Dkt. Dugange alisema mito ya Mfizigo na Mhuva iliyopo katika jimbo hilo ni moja ya maeneo ambako hufanyika shughuli za uchimbaji mdogo wa madini katika maeneo ya pembezoni mwa mito hiyo.

Alisema katika kuhakikisha mito hiyo inatunzwa na kuzuia uchafuzi wake kutokana na shughuli za uchimbaji madini, Serikali mwaka 2025 ilichukua sampuli za maji ya mito hiyo kwa ajili ya kupima ikiwa kuna uchafuzi wa kemikali zitokanazo na uchimbaji na uchenjuaji wa madini.

Dkt. Dugange alifafanua kuwa matokeo ya vipimo vya sampuli hizo vilionesha kuwa kuna kemikali za chuma na manganizi. 

“Kemikali zilizobainika kuwepo zinatokana na miamba iliyo kuwa inachimbwa na sio kwamba zinatokana na matumizi ya kemikali za kuchenjulia madini kama zebaki. Aidha kemikali hizi zilibainika kutokuwa na madhara kwa binadamu na bionuwai,” alisisitiza.

Katika swali la nyongeza la Mbunge wa Kakonko Mhe. Alan Mvano aliyetaka kujua hatua za kunusuru mito, Mhe. Dugange alisema Serikali inahakikisha suala la uchimbaji linaendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Uhifadhi namba 191 ambapo kipaumbele ni kuweka mazingira wezeshi na utunzaji wa mazingira.
Posted by MROKI On Tuesday, January 27, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi akipata mti nje ya jengo la Wizara leo tarehe 26 Januari, 2026 ikiwa zoezi la kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wake wa kizalendo wa kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwa vitendo vya kulinda mazingira. 

Katibu Mkuu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. John Jingu akipata mti nje ya jengo la Wizara leo tarehe 26 Januari, 2026 ikiwa zoezi la kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wake wa kizalendo wa kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwa vitendo vya kulinda mazingira. 
Mmoja wa Mzee Dijina Ndilito mti nje ya jengo la Wizara leo tarehe 26 Januari, 2026 ikiwa zoezi la kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wake wa kizalendo wa kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwa vitendo vya kulinda mazingira. 

****************
Na Raymond Mushumbusi WMJJWM- Dodoma
Baadhi ya Wazee kutoka Baraza la Wazee Mkoa wa Dodoma wameshirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum katika zoezi la upandaji Miti kwa lengo la kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wake wa kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwa vitendo vya kulinda mazingira.

Wakizungumza mara baada ya zoezi hilo wamempongeza Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Uongozi wake mahiri na thabiti katika kuliongoza taifa kwa misingi ya amani na utulivu.

"Tunampongeza Rais Samia kwa hatua yake ya kuitumia Siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake kuhamua kupanda Miti ili kuleta hamasa kwa watanzania katika kuyapenda na kuyatunza mazingira" wamesema Wazee hao.

Akiongoza zoezi hilo Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi Januari 27, 2026 amesema lengo ni kuenzi maono ya Rais Samia la kutunza mazingira yanayotuzunguka.

Naibu Waziri Mahundi amempongeza Rais Dkt. Samia kwa uongozi wake kwa kuendelea kudhihirisha kiongozi maono, mbunifu wake na namna anavyojali maslahi ya Taifa.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. John Jingu amesema Wizara imeshirikiana na kundi la Wazee kuwakilisha Makundi Maalum mengine yanayosimamiwa na Wizara katika zoezi hilo ambalo lina lengo kulinda na kutunza mazingira.

Zoezi la upandaji Miti mbele ya Ofisi ya Wizara Mtumba Jijini Dodoma limehusisha Kundi la Wazee Mkoa wa Dodoma, Menejimenti na Watumishi wa Wizara hiyo.
Posted by MROKI On Tuesday, January 27, 2026 No comments
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange akipanda mti katika eneo la Mji wa Serikali Mtumba kwa ajili kuadhimisha Kumbukizi ya Siku ya Kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Januari 27, 2026 jijini Dodoma.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange akipanda mti katika eneo la Mji wa Serikali Mtumba kwa ajili kuadhimisha Kumbukizi ya Siku ya Kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Januari 27, 2026 jijini Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi akipanda mti katika eneo la Mji wa Serikali Mtumba kwa ajili kuadhimisha Kumbukizi ya Siku ya Kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Januari 27, 2026 jijini Dodoma.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange akikata keki maalumu ya kumpongeza na kuadhimisha Kumbukizi ya Siku ya Kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, iliyofanyika sanjari na zoezi la upandaji wa miti katika eneo la Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma leo Januari 27, 2026 jijini Dodoma. Anayeshuhudia kulia ni Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange akizungumza na viongozi, watumishi wa Serikali na wananchi wakati wa zoezi la upandaji wa miti kwa ajili kuadhimisha Kumbukizi ya Siku ya Kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, lililofanyika katika eneo la Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma leo Januari 27, 2026 jijini Dodoma.
*****************
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange ametoa rai kwa kila Mtanzania kupanda mti angalau mmoja kila mwaka anapoadhimisha kumbukizi ya siku ya kuzaliwa ili kuleta chachu katika hifadhi endelevu ya mazingira.
 
Ametoa rai hiyo wakati akiongoza zoezi la upandaji wa miti kuadhimisha Kumbukizi ya Siku ya Kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Januari 27, 2026 katika Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.
 
Dkt. Dugange alisema misitu ni uhai hivyo Viongozi wa ngazi mbalimbali na Watanzania kwa ujumla wanapaswa kuwa na utamaduni wa kupanda miti na kuitunza hatua itakayosaidia kuhifadhi mazingira na kukabailiana na mabadiliko ya tabianchi.
 
“Watanzania tupo zaidi ya watu milioni 61 kila moja wetu akiiga mfano wa Rais wetu kupanda angalau mti mmoja kila mwaka anaposherehekea siku ya  kuzaliwa, tutapanda miti milioni 61 na baada ya miaka kumi tutapanda miti bilioni 61,” alisisitiza.
 
Akizungumzia zoezi la upandaji wa miti, Dkt. Dugange alisema ni hatua ya kuungana na Rais Dkt. Samia ambaye ni kinara katika utunzaji wa mazingira na kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais inayo heshima ya kuungana naye kwa kumpongeza na kumtakia heri.
 
Naibu Waziri aliongeza kuwa zoezi la upandaji wa miti litakuwa endelevu kwa kuwa maeneo ya yanayotakiwa kupandwa miti bado yapo na miti hiyo inapatikana kwa urahisi.
 
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Mazingira Bw. Thomas Chali alisema
pamoja na mambo mbalimbali lengo la kufanya zoezi la upandaji wa miti katika eneo hilo ni kurejesha hali nzuri ya mazingira kwa ajili ya kupumzikia.
 
Alisema eneo hilo lenye ukubwa wa hekta mbili ni bustani ya miti ambayo Ofisi ya Makamu wa Rais ilipatiwa mwaka 2023 na kulifanyia usafi na kuanza kupanda miti 1665 ambayo hata hivyo kutokana na ukame ni miti 982 pekee ndio ilistawi.
 
Hivyo, Bw. Chali alisema Ofisi imeendelea kulitunza eneo hilo la bustani kwa kushiriki kampeni za upandaji wa miti ikiwemo ya kuadhimisha Siku ya Kuzaliwa Mhe. Rais Dkt. Samia ambaye alizindua Kampeni ya Kukijanisha Dodoma alipokuwa Makamu wa Rais mwaka 2017.
 
Nae Kaimu Naibu Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Dkt. Zainab Bungwa alisema inawezekana kuifanya nchi isiwe jangwa kwa kupanda miti kwa wingi.
 
Alisema shughuli za kibinadamu huchangia uharibifu wa mazingira na hata kutishia jangwa. Hivyo suluhisho ni kujenga mazoea ya kupanda miti badala ya kuikata.

Dk Bungwa aliongeza kuwa hadi sasa Tanzania ina jumla ya misitu 465 ambayo inamilikiwa na Serikali Kuu, Serikali za Mitaa, Vijijini na mamlaka zingine na kati ya hiyo, 26 ni hifadhi za misitu ya asili.
Posted by MROKI On Tuesday, January 27, 2026 No comments

Mfuko wa kimataifa wa uwekezaji Sino American Global Fund (SinoAm LLC) umeonesha nia ya kuwekeza hadi Dola za Marekani bilioni 5 nchini Tanzania katika miradi mikubwa ya kimkakati, hususan katika sekta za miundombinu, usafirishaji, nishati, teknolojia, huduma za kifedha na maendeleo ya viwanda.

Nia hiyo iliwasilishwa rasmi wakati wa mkutano kati ya uongozi wa SinoAm LLC na Prof. Kitila Alexander Mkumbo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, uliofanyika jijini London, Uingereza, pembezoni mwa ziara rasmi ya Waziri huyo nchini humo.

Akizungumza kwa niaba ya SinoAm LLC, Bw. Najib Choufani, Mwenyekiti wa Mfuko huo, alieleza kuwa mfuko huo umejipanga kuwekeza kiasi kinachoweza kufikia USD bilioni 5 nchini Tanzania kwa awamu, kupitia miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), sambamba na vipaumbele vya maendeleo ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Bw. Choufani alibainisha kuwa SinoAm LLC imefanya tathmini ya kina ya mazingira ya uwekezaji nchini Tanzania na kubaini fursa zenye tija kubwa, ikiwemo ujenzi na uendeshaji wa barabara za kisasa za kulipia (toll expressways), miradi ya reli ya kiwango cha kimataifa (SGR), pamoja na miundombinu muhimu ya uchukuzi na nishati inayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ushindani wa Tanzania kikanda.

Katika mkutano huo, uongozi wa SinoAm LLC pia uliambatana na Bw. Tarek Choufani, Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko huo, ambaye alieleza kuwa SinoAm ina uzoefu mpana wa kimataifa katika kusimamia miradi mikubwa ya miundombinu na iko tayari kuleta si tu mitaji mikubwa, bali pia utaalamu wa kiufundi, mifumo ya kisasa ya usimamizi na mbinu bora za kimataifa nchini Tanzania.

Kwa upande wake, Waziri Mkumbo aliipongeza SinoAm LLC kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kuwekeza kiasi kikubwa cha mitaji nchini Tanzania, akibainisha kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wakubwa wa kimataifa. Alisisitiza kuwa Tanzania ina utulivu wa kisiasa, sera rafiki za uwekezaji, na dira ya muda mrefu ya maendeleo inayotoa uhakika na ulinzi kwa uwekezaji wa kimkakati.

Posted by MROKI On Tuesday, January 27, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo