Nafasi Ya Matangazo

October 04, 2015



Mchungaji Christopher Mtikila amefariki hii leo katika ajali baada ya gari alilokuwa akisafiria kuacha njia na kupinduka eneo la Msolwa-Chalinze mkoani Pwani.

Mtiklila alikuwa kiongozi wa chama cha upinzani Tanzania cha Democratic Party (DP).

Mtikila alizaliwa Ludewa Mkoani Njombe, kusini mwa Tanzania, mwaka 1950. Pamoja na shughuli za siasa, Mchungaji Mtikila ni mwanzilishi na mkuu wa kanisa la Kipentekoste la Full Salvation Church.

Mchungaji Mtikila amekuwa pia alijihusisha na harakati za haki za binadamu kwa kupitia kitengo cha haki za binadamu cha kanisa hilo kiitwacho Liberty Desk.

Mwanzoni mwa miaka ya 90, mchungaji Mtikila alijipatia umaarufu mkubwa katika siasa za Tanzania kutokana na uwezo wake mkubwa wa kuongea, upinzani wake dhidi ya muundo wa muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar, madai yake kuhusu uhujumu wa uchumi unaofanywa na wahindi (ambao anawaita Magabacholi), na kesi mbalimbali za kikatiba alizokuwa akifungua katika mahakama za Tanzania.

Kwa muda mrefu chama chake cha DP hakikuweza kupata usajili wa kudumu kutokana na kukataa kwake kutambua Zanzibar.

Alikuwa akisisitiza kuwa chama chake ni cha Tanganyika na sio Tanzania. Hata hivyo Mtikila alibadili msimamo wake katika miaka ya karibuni kwa kukubali kutafuta wanachama toka Zanzibar (kama sheria ya uchaguzi inavyotaka) na hivyo chama chake kuweza kupata usajili wa kudumu.

Mwaka 1997, Mbunge wa Ludewa kwa tiketi ya CCM wakati huo, Horace Kolimba aliitwa na Kamati Kuu ya chama chake mjini Dodoma kwenda kujibu mashtaka ya ndani ya chama juu ya kauli ambazo alikuwa akizitoa kwamba “CCM imepoteza mwelekeo”, baadhi ya viongozi wa chama chake walimchukulia kama msaliti na wengine wakimuona kama mtu aliyethubutu kusema ukweli bila kumhofia Nyerere. Hata hivyo, Kolimba alifariki hukohuko Dodoma katika siku ambazo alikuwa akihojiwa.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilipotangaza uchaguzi mdogo, ndipo Mtikila alikihama chama chake cha DP akajiunga na Chadema na kuomba ridhaa ya kugombea. Mtikila ni mzaliwa wa Ludewa na alifanya hivyo kwa sababu chama chake cha DP kilikuwa kimenyimwa usajili.

Uchaguzi ulifanyika Mei 25, 1997 na kumpa ushindi mgombea wa CCM Profesa Chrispin Haule Che Mponda ambaye alipata kura 20,111 dhidi ya 8,386 za Mtikila. Mgombea wa NCCR ambayo haikuwa imejijenga vilivyo Ludewa, Barnabas Kidulile, alipata kura 1,271.

Baada ya kushindwa uchaguzi huo, Mtikila alisikika akihitilafiana na Chadema hadharani huku akitoa shutuma nzitonzito, akafukuzwa kwenye chama hicho na ndipo akaendelea kuwekeza nguvu kwenye mipango ya kukamilisha usajili wa chama chake.

Mbio za urais

Mtikila alianza harakati za kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 2005 kwa tiketi ya DP. Alikuwa kati ya wagombea 10 katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huo. Katika uchaguzi huo, alipata asilimia 0.27 ya kura zote, akiwa nyuma ya Jakaya Kikwete wa CCM (asilimia 80.28), Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF (asilimia 11.68), Freeman Mbowe wa Chadema (asilimia 5.88), Augustine Mrema wa TLP (asilimia 0.75) na Dk Sengondo Mvungi wa NCCR (asilimia 0.49).

Katika Uchaguzi Mkuu unaotaraji kufanyika Oktoba 25 mwaka huu Mtikila kupitia DP, alichukua fomu lakini alishindwa kutimiza masharti ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi na jinalake kuondolewa katika orodha ya wagombea Urais.

Kesi za kikatiba ambazo amewahi kufungua ni pamoja kesi ya kutaka wagombea binafsi kuruhusiwa katika uchaguzi Tanzania, wananchi wa Tanzania Bara kuruhusiwa kwenda Zanzibar bila pasipoti, na vyama vya siasa kuruhusiwa kufanya mikutano bila kuomba kibali toka kwa Mkuu wa Wilaya na Polisi.

Mtikila alifungwa kwa mwaka mmoja mwaka 1999 baada ya kupatikana na hatia ya kutoa maneno ya kashfa dhidi ya aliyekuwa katibu mkuu wa CCM, marehemu Horace Kolimba.

Mwaka 2004 alihukumiwa kifungo kilichosimamishwa cha miezi sita kwa kutoa maneno ya kashfa dhidi ya mkuu wa polisi wa wilaya ya Ilala.

Mchungaji Christopher Mtikila, mwaka huu mwezi March alifungua kesi ya kikatiba namba 14 ya mwaka 2015 katika Mahakama Kuu ya Tanzania kupinga muswada wa mabadiliko ya sheria kwa ajili ya kuitambua rasmi Mahakama ya Kadhi.
Posted by MROKI On Sunday, October 04, 2015 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo